Alimu mkubwa Tunisia: Fatwa za mamufti wa Kiwahabi, zinalenga kuusambaratisha Uislamu
Alimu mmoja wa ngazi ya juu wa Kiislamu nchini Tunisia, amesema kuwa fatwa za upotoshaji za mamufti wa Saudia, zinaelekea kuuangamiza umma wa Kiislamu.
Sheikh Shubair Ibn Hassan, alimu mkubwa wa Tunisia amesisitiza kuwa, ugaidi unaoshuhudiwa hii leo duniani, ni matokeo ya siasa chafu za utawala wa kifalme wa Saudia na fatwa za mamufti wa nchi hiyo. Sambamba na kubainisha kwamba katika kipindi cha muongo mmoja uliopita mamufti wa Saudia wamekuwa na nafasi kubwa katika kuibua fitina na tofauti baina ya Waislamu duniani. Sheikh Shubair ametoa mfano wa hukumu za 'bidaa' kuwalenga wapinzani wao kwa kuhalalisha mauaji dhidi yao na kusema kwamba hukumu hizo ni fitina kubwa ambayo iliibuliwa na Mawahabi hao kati ya Waislamu duniani.

Aidha alimu huyo wa Tunisia amebainisha kwamba, hii leo ardhi takatifu za Makkah na Madina zimekaliwa kwa mabavu na utawala wa Aal-Saud na kwamba hakuna mtu anayepinga suala hilo. Sheikh Shubair Ibn Hassan amesema kuwa, fatwa potofu za Wasaudi zinatolewa kuwalenga watu ambao wanapinga dhulma za watawala wa Aal-Saud kama ambavyo pia wanawaona Waislamu wengine duniani kuwa ni washirikina isipokuwa wafuasi pekee wa Uwahabi.

Hii sio mara ya kwanza kwa maulama mbalimbali duniani kulaani na kukemea fatwa potofu za maulama wa Kiwahabi ambazo, mbali na kuzalisha wimbi la ugaidi, zimesababisha pia mauaji na umwagaji mkubwa wa damu za watu wasio na hatia katika maeneo tofauti ya dunia.