Libya yaiomba Russia iisaidie kutatua migogoro yake
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i47319-libya_yaiomba_russia_iisaidie_kutatua_migogoro_yake
Msemaji wa Jeshi la Taifa la Libya ameiomba serikali ya Russia iingilie mgogoro wa Libya kwa ajili ya kuutatua.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Aug 08, 2018 23:54 UTC
  • Libya yaiomba Russia iisaidie kutatua migogoro yake

Msemaji wa Jeshi la Taifa la Libya ameiomba serikali ya Russia iingilie mgogoro wa Libya kwa ajili ya kuutatua.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Sputnik, Ahmed al Mismari, msemaji wa Jeshi la Taifa la Libya amesema, utatuzi wa mgogoro wa nchi hiyo unahitajia msaada wa Russia na hasa wa Rais Vladimiri Putin mwenyewe wa nchi hiyo.

Amesema, kuna wajibu kwa nchi zilizo na mkono katika mgogoro wa Libya hasa Uturuki, Qatar na Italia kujitoa katika mgogoro huo ndipo utaweza kutatuliwa. Hata hivyo amasema, kuna wajibu wa kutumiwa uzoefu wa kidiplomasia wa Russia kutatua mgogoro wa nchi hiyo.

Jenerali Khalifa Haftar (wa pili kushoto) akiwa ziarani mjini Moscow, Russia

 

Ahmed al Mismari amegusia pia ziara ya hivi karibuni ya Jenerali Khalifa Haftar, kamanda wa vikosi vya Jeshi la Taifa la Libya huko Moscow na kusisitiza kuwa, jeshi hilo litaendeleza uhusiano wake na Russia.

Libya ilitumbukia kwenye machafuko mwaka 2011 baada ya Marekani na shirika la kijeshi la nchi za Magharibi NATO kuivamia kijeshi nchi hiyo katika kampeni za kuungasha utawala wa Kanali Muammar Gaddafi.

Tangu wakati huo hadi hivi sasa nchi hiyo imeshindwa kuwa na utulivu wa angalau siku na mivutano baina ya makundi mbalimbali yanayoungwa mkono na madola ajinabi ni sababu kuu ya kukosekana utulivu huko Libya.