Sudan Kusini yaamua kufunga balozi zake kadhaa nje ya nchi
Sudan Kusini imesema kuwa inapamga kufunga balozi zake katika miji mikuu sita duniani zikiwemo balozi zake zilizoko Saudi Arabia, Imarati na Norway.
Taarifa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan Kusini inaeleza kuwa Juba inapanga kuzifunga rasmi hivi karibuni balozi zake huko Ufaransa, Israel, Saudi Arabia, Imarati, Norway na Ghana. Taarifa hiyo imeongeza kuwa Juba imechukua uamuzi huo kutokana na Sudan Kusini kukabiliwa na matatizo ya kifedha.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan Kusini mwishoni mwa wiki iliyopita pia ilihitimisha ushirikiano wake na wanadiplomasia 40.
Nchi hiyo ilijitenga na Sudan mwaka 2011 kwa uungaji mkono wa Marekani, nchi nyingine za Magharibi na taasisi za kimataifa. Nchi hiyo changa zaidi barani Afrika licha ya kuwa na utajiri wa mafuta na madini lakini inakabiliwa na matatizo makubwa ya kiuchumi, kijamii na mivutano ya ndani. Hii ni katika hali ambayo mashirika makubwa ya mafuta duniani yanaendesha shughuli zake huko Sudan Kusini; na asilimia 95 ya mapato ya nchi hiyo yanatokana na uuzaji nje mafuta.