Watu 25 wauawa kwenye hujuma ya wanamgambo nchini Nigeria
Watu 25 wameuawa katika shambulizi lililofanywa na kundi la watu waliokuwa na silaha jimboni Sokoto, kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa ya Polisi ya Nigeria, washambuliaji wanne waliotekeleza hujuma hiyo wamekamatwa na miongoni mwao kuna mwanamke.
Kamishna wa polisi wa jimbo hilo Bw. Ibrahim Kaoje amesema shambulizi hilo lililotokea Jumamosi usiku na walioathirika zaidi ni wakazi wa vijiji vitatu vya Kalhu, Tsage na Geeri vilivyoko kwenye eneo la Rabah, kaskazini mwa Nigeria. Washambulizi hao pia wameiba ng'ombe, mbuzi, na vitu kadhaa vya thamani.
Rabah ni kati ya maeneo ya kaskazini magharibi mwa Nigeria ambayo yamekumbwa na hujuma za watu wenye silaha katika miezi ya hivi karibuni.
Kwa uchache watu 108 wameuawa jimboni Sokoto kuanzia mwishoni mwa mwaka 2018 katika mashambulizi ya wanagambo.
Gavana wa Jimbo la Sokoto Aminu Tambuwal amehudhuria mazishi ya waliouawa na ameahidi kuwa serikali itachukua hatua za kusitisha mauaji hayo ya kinyama.