Mamia wapoteza makazi baada ya moto kuteketeza eneo kubwa Sudan Kusini
Mamia ya watu wamepoteza makazi yao Sudan Kusini katika eneo la Nzara baada ya kukumbwa na janga la moto wa nyika ambao umeteketeza takribani maili tano mraba katika jimbo la Equatoria Magharibi.
Mpango wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS umesema moto huo umeteketeza nyumba za Tukul ambazo ni nyumba za asili za eneo hilo, mifugo na kupoteza maisha ya mtu mmoja.
Afisa wa UNMISS Stella Folasade Abayomi, ambaye anahusika na masuala ya jamii mjini Yambio anasema madhara ya moto huo yanatisha.
Ameongeza kuwa idadi kubwa ya watu wametawanywa kufuatia janga hilo huku wengi wakiripopti kupoteza mali zao na kimsingi vyanzo vyao vya mapato maana hapo wengi ni wakulima.

Hali kadhalika amesema mashamba yamechomeka na wakazi wamepoteza vyakula vyao vyote katika maghala.
Afisa huyo wa Umoja wa Mataifa ametoa wito wa misaada ya haraka ya kibinadamu ili kuwasaidia watu kwa kuwapatia makazi ya muda, mahema, chakula na bila shaka vitu vingine ambavyo si chakula.