Bunge la Kiarabu laiunga mkono Morocco katika hitilafu zake na Uhispania
Bunge za Nchi za Kiarabu limetangaza katika taarifa yake kuwa linaiunga mkono Morocco kuhusu hitilafu zilizojitokeza kati ya nchi hiyo na Uhispania.
Bunge la Kiarabu limetoa taraifa yake huko Cairo mji mkuu wa Misri na kutangaza kuwa, linaiunga mkono Morocco kuhusu hitilafu zilizojitokeza kati ya nchi hiyo na Uhispania. Bunge hilo aidha limekosoa tuhuma zilizotolewa na Bunge la Ulaya dhidi ya Rabbat kuhusu mapambano dhidi ya wahamiaji haramu wanaoelekea Ulaya.
Wakati huo huo Bunge la Ulaya pia limetoa taarifa likiituhumu Morocco kuwa inakiuka sheria zinazohusiana na wahamiaji haramu wanaoelekea Ulaya kwa ajili ya kutafuta hifadhi na hatua ya nchi hiyo ya kuwatumia watoto katika uwanja huo.
Algeria, Syria na Lebabon zimekataa kuiunga mkono taarifa hiyo ya Bunge la Kiarabu.
Mgogoro katika uhusiano wa Uhispania na Morocco ulianza Novemba 21 mwaka jana kufuatia hatua ya rais wa wakati huo wa Marekani Donald Trump ya kutambua rasmi mamlaka ya Morocco huko Sahara Magharibi. Mgogoro huo ulipamba moto zaidi baada ya Ibrahim Ghali Katibu Mkuu wa Harakati ya Polisario kuelekea Uhispania mapema mwaka huu kwa ajili ya kutibiwa ugonjwa wa corona.
Kitendo hicho kiliipelekea Rabat imwite nyumbani balozi wake mjini Madrid na hivyo kuchochea zaidi mvutano wa kuainisha alama za mipaka ya baharini kati ya nchi mbili hizo.