Sisitizo la Iran katika kuimarisha uhusiano na Tanzania
Hossein Amir-Abdollahian, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran aliwasili nchini Tanzania Jumatano usiku na kusema kwamba kunatayarishwa ramani ya njia kuhusiana na kuimarisha uhusiano wa Iran na Tanzania ili mchakato huo uchukue mkondo wa kasi.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran aliwasili katika uwanja wa ndege wa Dar es Salaam nchini Tanzania akitokea Bamako, mji mkuu wa Mali. Punde baada ya kuwasili Amir-Abdollahian alikaribishwa rasmi na Liberata Mulamula, Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Iranpress, Amir-Abdollahian amezungumza na waandishi wa habari katika uwanja wa ndege wa Dar es Salaam na kusema kwamba wakati wa mkutano na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bi Samia Suluhu Hassan, atamkabidhi mwaliko rasmi wa kuitembelea Iran kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Seyed Ebrahim Raisi.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema katika ujumbe wake, ameandama na wafanyabiashara, wamiliki wa viwanda na wajumbe wa sekta za serikali kwa lengo la kushiriki katika vikao muhimu jijini Dar es Salaam.
Amir-Abdollahian ameashiria safari yake ya Zanzibar na kusema atafanya mkutano wa kibiashara na vikao rasmi na viongozi wa eneo hilo.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania kwa upande wake ameeleza kufurahishwa kwake na uwepo wa Amir -Abdollahian na ujumbe wake nchini Tanzania na kuongeza kuwa Watanzania wamekuwa wakisubiri kwa muda mrefu safari hii ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran nchini Tanzania.
Liberata Mulamula amesema uhusiano kati ya Tanzania na Iran ni mzuri sana na wa karibu na kuelezea matumaini kuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran atarefusha safari yake nchini Tanzania.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alitembelea Mali kabla ya Tanzania. Nchini Mali, Amir-Abdollahian alikutana na kuzungumza na mkuu wa serikali ya mpito ya nchi hiyo.
Pia katika safari hii kikao cha kwanza cha Kamisheni ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Jamhuri ya Mali kilifanyika chini ya uenyekiti wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi hizo mbili, na mwishoni mwa kikao hicho hati ilitiwa saini na ikaamuliwa kuwa mkutano ujao utafanyika Tehran.