Kuongezeka mivutano katika uhusiano wa Rwanda na Burundi
Hali ya mvutano katika uhusiano wa Rwanda na Burundi imeongezeka baada ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda bi Louise Mushikiwabo kusema kuwa nchi yake iko tayari kukabiliana na vitisho vya kiusalama kutoka Burundi.
Louise Mushikiwabo amesisitiza leo katika kikao na waandishi wa habari kuwa raia wa Burundi karibu 1500 wamefukuzwa nchini humo, hata hivyo watu hao wamerejea tena nchini kupitia njia haramu, kitendo ambacho kitaathiri hali ya usalama.
Mushikiwabo ameongeza kuwa baadhi ya wakimbizi kutoka Burundi ambao waliingia Rwanda kinyume cha sheria wameongezeka na kwamba hali hiyo itaisababishia Rwanda changamoto za kiusalama. Hii ni katika hali ambayo kabla ya hapo pia uhusiano wa nchi mbili hizo haukuwa mzuri. Burundi inaituhumu jirani yake Rwanda kuwa inawaunga mkono waasi wa Burundi. Wakati huo huo Paschal Nyabenda mkuu wa chama tawala Burundi CNDD-FDD amezituhumu baadhi ya serikali za Ulaya kuwa zinampatia silaha na kumfadhili kifedha Rais wa Rwanda. Burundi imetumbukia katika mgogoro wa kisiasa na hali ya machafuko tangu mwezi Aprili mwaka jana.