Khatibu: Kimbunga cha al-Aqsa kimefichua nidhamu kadhaa za kisiasa duniani
(last modified Fri, 15 Dec 2023 12:05:27 GMT )
Dec 15, 2023 12:05 UTC
  • Khatibu: Kimbunga cha al-Aqsa kimefichua nidhamu kadhaa za kisiasa duniani

Khatibu wa muda wa Swala ya Ijumaa ya leo hapa mjini Tehran amesema Operesheni ya Kimbunga cha Al-Aqsa na muqawama wa Wapalestina wa Gaza vimefichua kuwepo nidhamu na miundo kadhaa ya kisiasa duniani, sambamba na kuonyesha kuwepo stratejia mpya ya kambi ya muqawama katika eneo.

Hujjatul-Islam Mohammad Hassan Aboutorabifard ameeleza kuwa, "Watu wa Gaza wameibua enzi za kipekee katika historia ya mapambano na kujitoa muhanga taifa la Palestina."

Amebainisha kuwa, jinai za Israel huko Gaza zimefichua unafiki na undumakuwili wa Marekani na washirika wake wa Ulaya na wavamizi Wazayuni.

Hujjatul-Islam Aboutorabifard amesema Gaza leo hii imeanika wazi unafiki na ukatili wa Marekani machoni pa jamii ya kimataifa kwa kutumia 'mauzo ya nje' ya bidhaa zake kama uhuru, haki za binadamu na demokrasia ya Magharibi.

"Kambi ya binadamu katika mizani ya jografia ya dunia imeundwa mkabala wa thamani zisizo za kiutu na za kibinafsi za watawala wa Magharibi," ameongeza Aboutorabifard.

Ikumbukwe kuwa, katika kukabiliana na jinai za Wazayuni, vikosi vya muqawama vya Palestina vilianzisha Operesheni ya Kimbunga cha al-Aqsa dhidi ya ngome za utawala wa Kizayuni  wa Israel kuanzia Oktoba 7, 2023.

Wanamuqawama wa Palestina

Kwa mujibu wa ripoti ya Wizara ya Afya ya Palestina, zaidi ya watu 18,800 wameuawa shahidi na wengine takriban 50,000 wamejeruhiwa katika jinai za utawala wa Kizayuni katika Ukanda wa Gaza tokea Oktoba 7.

Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Khatibu wa Swala ya Ijumaa ya leo mjini Tehran ameshiria shambulizi la kigaidi la jana usiku katika makao ya jeshi la polisi huko Rask, mkoani Sistan na Baluchistan kusini mashariki mwa Iran na kusema kuwa: Baadhi ya walinzi bora wa mipakani wa Iran wameuawa shahidi katika hujuma hiyo ya mamluki wa maadui.

Watu 12 waliuawa shahidi katika shambulio hilo la kigaidi lililolenga makao ya jeshi la polisi huko Rask. 

Ameongeza kuwa, anatumai vyombo vya usalama na intelijensia vya Iran vitawatambua na kuwaadhibu wahusika wa jinai hiyo. Tayari genge la kigaidi la Jaishul-Dhulm limekiri kuhusika na shambulizi hilo.