Qalibaf ataka ushirikiano wa vikwazo dhidi ya Israel na kuundwa nchi huru ya Palestina
(last modified Wed, 14 May 2025 11:39:47 GMT )
May 14, 2025 11:39 UTC
  • Qalibaf ataka ushirikiano wa vikwazo dhidi ya Israel na kuundwa nchi huru ya Palestina

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amezitaka nchi za Kiislamu kuuwekea vikwazo vya kisiasa, kiuchumi na kijeshi utawala wa Kizayuni wa Israel ili kukomesha mauaji ya kimbari huko Gaza.

Muhammad Baqir Qalibaf amesema hayo katika hotuba yake kwenye Mkutano wa 19 wa Umoja wa Mabunge ya Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (PUIC) na kutoa wito wa kuanzishwa taifa huru la Palestina mji mkuu wake ukiwa Baytul-Muqadda sambamba na kudhamini haki ya kurejea kwa Wapalestina.

Spika wa Bunge la Iran ameeleza kuwa, "Leo mishipa ya uhai na kiuchumi ya utawala wa Kizayuni inapitia katika baadhi ya nchi za Kiislamu, hivyo wakati umefika kwa nchi za Kiislamu kuchukua uamuzi wa pamoja wa kukomesha mzingiro wa Gaza."

Spika Qalibaf amesema: Katika wakati wetu, tunakabiliwa na mrundikano wa changamoto, misukosuko na mashaka, mabadiliko ya haraka, kupanda kwa ushuru wa forodha, mabadiliko ya hali ya hewa na migogoro ya mazingira, kuporomoka kwa biashara ya kimataifa, kuenea kwa vita na ukosefu wa usalama, na hata mauaji ya kimbari yaliyoratibiwa.

Mkutano wa 19 wa Wabunge wa Umoja wa Ushirikiano wa Kiislamu (PUIC) unafanyika mjini Jakarta kuanzia Mei 12 hadi 15 chini ya mada "Utawala Bora na Taasisi Imara kama Nguzo za Ustahimilivu.