Wabunge wa Iran waziasa nchi 44 ziiwekea Israel vikwazo
Wanachama wa Kamati ya Mahakama na Sheria ya Bunge la Iran wametoa wito kwa makumi ya nchi duniani kuchukua hatua za kuiwekea Israel vikwazo kutokana na utawala huo "kukiuka kanuni za kimataifa na haki za binadamu."
Katika barua iliyotumwa kwa mabunge ya mataifa 44 duniani jana Alkhamisi, wabunge hao wa Iran wamezitaka kamati za sheria za mabunge hayo kulaani uchokozi haramu wa mwezi uliopita wa Israel na Marekani dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu na kuuarifu Muungano wa Mabunge ya Muungano (IPU) kuhusu uamuzi wao.
Vilevile wameyataka mabunge hayo kuweka kwenye ajenda zao mchakato wa kutunga sheria kwa ajili ya kuchukua hatua za vikwazo dhidi ya utawala dhalimu wa Kizayuni.
"Kadhalika, kamati za sheria zimetakiwa kuweka uchunguzi wa jinai za Israel ndani ya utawala na mamlaka za kisheria za nchi zao, ili kuzuia kutoadhibiwa kwa utawala wa Kizayuni na Marekani, na kukomesha uchochezi wa Israel duniani," imesema barua hiyo iliyotiwa saini na Mohammad Sargazi, Mkuu wa Kamati ya Mahakama na Sheria ya Bunge la Iran.
Mnamo Juni 13, Israel ilianzisha uchokozi wa wazi na usio na msingi dhidi ya Iran, na kuua shahidi watu wasiopungua 1,060, wakiwemo makamanda wa ngazi za juu wa kijeshi, wanasayansi wa nyuklia na raia wa kawaida.
Marekani pia iliingia vitani Juni 22 na kushambulia kwa mabomu maeneo matatu ya nyuklia ya Iran katika ukiukaji mkubwa wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa, sheria za kimataifa na Mkataba wa Kuzuia Uzalishaji na Uenezaji wa Silaha za Nyuklia (NPT).
Katika kujibu chokochoko hizo, Vikosi vya Wanajeshi vya Iran vililenga maeneo ya kimkakati katika maeneo yote yanayokaliwa kwa mabavu na Israel, na pia kambi ya anga ya al-Udeid huko Qatar, kambi kubwa zaidi ya kijeshi ya Marekani Asia Magharibi. Tarehe 24 Juni, Iran, kupitia operesheni zake za kulipiza kisasi zilizofanikiwa dhidi ya utawala wa Israel na Marekani, iliweza kusimamisha mashambulizi hayo ya kigaidi.