Ayatullah Hashemi Rafsanjani amezikwa leo
Mwili wa marehemu Ayatullah Hashemi Rafsanjani, Mkuu wa Halmashauri ya Kuainisha Maslahi ya Mfumo wa Kiislamu wa Iran umezikwa leo katika haram ya mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Imam Khomeini (MA).
Mwili wa Sheikh Hashemi Rafsanjani, ulisindikizwa na mamia ya maelfu ya waombolezaji wa Iran ya Kiislamu kutoka Chuo Kikuu cha Tehran kuelekea haram toharifu ya Imam Khomeini (MA).
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ndiye aliyeongoza Sala ya Maiti ya kumsalia marehemu Ayatullah Rafsanjani katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Tehran. Viongozi wa ngazi za juu za nchini, wakiwemo wa serikali na vikosi vya ulinzi pamoja na mabalozi kadhaa wa nchi za nje walioko mjini Tehran walishiriki kwenye shughuli ya maziko ya Sheikh Hashemi Rafsanjani.
Mkuu wa Halmashauri ya Kuainisha Maslahi ya Mfumo wa Kiislamu wa Iran aliaga dunia Jumapili usiku kutokana na matatizo ya moyo katika hospitali moja ya mjini Tehran…/