Iran yalaani shambulizi ya kigaidi karibu na Husainiya ya Imambargah
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amelaani shambulizi la kigaidi lililotokea katika eneo la Parachinar na kuua makumi ya watu waliokuwa wamekwenda kutelekeza ibada ya Swala ya Ijumaa.
Bahram Qassemi amelaani vikali shambulizi hilo lililolenga watu waliokwenda kutekeleza ibada ya Swala ya Ijumaa katika msikiti wa Waislamu wa madhehebu ya Shia kwenye mji wa Parachinar ambalo limeua watu wasiopungua 24 na kujeruhi wengine 90.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema maadamu baadhi ya nchi zinatumia lugha ya mabavu na mauaji badala ya lugha ya mantiki na mazungumzo kwa ajili ya kufikia malengo yao, hakuna matumaini ya kuweza kushinda na kung'oa mizizi ya ugaidi.
Qassemi amesisitiza kuwa, dawa mujarabu ya ugaidi kote duniani ni kuwa na azma imara ya kukata mishipa ya wale wote wanaofadhili na kuunga mkono misimamo mikali na makundi ya kigaidi na kuwepo ushirikiano wa kweli wa nchi zote katika uwanja huo.
Kundi la Taliban limetangaza kuwa ndilo lililohusika na shambulizi hilo lililotokea kwenye mlango wa wanawake wa kuingia kwenye eneo hilo la ibada.