Iran yalaani shambulio la kigaidi la Kabul, Afghanistan
Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amelaani vikali shambulio la kigaidi la kujitolea mhanga dhidi ya kituo kimoja cha masuala ya kiutamaduni na ofisi ya Shirika la Habari la Afghan Voice News katika mji mkuu wa Afghanistan, Kabul.
Bahram Qassemi ametoa mkono wa pole kwa serikali, taifa la Afghanistan na familia zilizopoteza ndugu zao waliouawa katika shambulio hilo la kigaidi na kubainisha kwamba, taifa la Iran lipo pamoja na familia na manusura wa shambulio hilo la kigaidi.
Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, kushambuliwa vituo vya kiutamaduni, vyombo vya habari, waandishi na wanafikra ambao wamekuwa wakifichua njama za fikra za kuchupa mipaka na utumiaji mabavu ni ishara ya wazi ya chuki na uadui mkubwa wa magaidi dhidi ya uhuru wa kujieleza, ufahamu, fikra na umoja wa wananchi wa Afghanistan.
Bahram Qassemi ameeleza kuwa, kuwa macho serikali na wananchi wa Afghanistan, umoja wa kaumu na makundi yote ya nchi hiyo na wakati huo huo kuweko ushirikiano wa nchi zote ndio siri ya kuweza kuwashinda magaidi wenye chuki, roho mbaya na wasio na huruma.
Kwa akali watu 41 wameuawa leo na makumi ya wengine kujeruhiwa kufuatia shambulio la kigaidi lililoutikisa mji mkuu wa Afghanistan, Kabul.