Zarif: Trump, Muhammad bin Salman na Netanyahu ni nembo ya ukatili duniani
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema kuwa Rais Donald Trump wa Marekani, Muhammad bin Salman mrithi wa kiti cha ufalme wa Saudi Arabia na Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel Benjamin Netanyahu ni nembo ya ukatili, uvunjaji wa haki, ukandamizaji na kutoaminiana duniani.
Akizungumza na waandishi wa habari leo kabla ya maadhimisho ya Siku ya Waandishi wa Habari yaani tarehe Nane Agosti, Muhammad Javad Zarif amesema kuwa leo hii watu wote duniani wanazungumzia suala la kutengwa Trump, Netanyahu na Bin Salman na kuongeza kuwa watu hao watatu wametengwa duniani kutokana na kutoheshimu mikataba ya kimataifa, kukiuka haki za watu wa Palestina na siasa zao za kutaka kuidhihirisha Iran kuwa ni tishio.
Zarif ameashiria pendekezo la viongozi wa Marekani la kutaka kufanya mazungumzo na Iran na kuongeza kuwa: Viongozi hao wa Marekani wameyapuuza makubaliano ya nyuklia ya JCPOA ambayo yaliungwa mkono na kuidhinishwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na nchi nyingi duniani na kisha Marekani ikajiondoa katika makubaliano hayo na kwamba licha ya mazingira haya nchi hiyo inadai kuwa wao ni watu wa mazungumzo!
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ameashiria pia jitihada za viongozi wa Marekani na utawala wa Kizayuni wa Israel za kutaka kuanzisha mawasiliano na wananchi wa Iran na kueleza kuwa iwapo mna uhusiano na wananchi wa Iran basi kwa nini vikwazo vya kwanza mlivyoweka vilikuwa vikwazo vya ndege?
Amesema tarehe Sita Agosti ni siku ya kurejesha vikwazo dhidi ya Iran na kwamba vikwazo hivyo havitakuwa na taathira kwa wananchi wa Iran bali zaidi viko vita vya kinafsi na kisaikolojia.