Qassemi: Uhusiano wa Iran na Afrika umesimama juu ya msingi wa kuheshimiana
Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Iran amesema kuwa uhusiano wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na nchi za Afrika daima umekuwa ukiheshimu mamlaka ya kitaifa ya kila nchi na kutilia mkazo suala la ustawi na ushirikiano.
Bahram Qassem ambaye alikuwa akijibu madai yaliyotolewa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Morocco, Nasser Bourita aliyesema kuwa Iran inafanya jitihada za kueneza ushawishi wake barani Afrika, amesema kuwa, madai ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Morocco hayana msingi na yanakariri tuhuma za maadui wa Iran wanaotaka kuzusha migawanyiko katika Umma wa Kiislamu.
Qassemi amesema uhusiano mzuri na safari za mara kwa mara za viongozi wa nchi za Afrika nchini Iran na kinyume chake ni ushahidi wa ushirikiano na uhusiano mzuri wa Iran na nchi muhimu za bara hilo.
Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Iran ameongeza kuwa: Inasikitisha kwamba madai yaliyotolewa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Morocco ambayo yamerushwa hewani na mojawapo kati ya vyombo vya habari vyenye fikra za kufurutu ada, vya kibaguzi zaidi na vya manazi mambo leo wa Marekani, yanakwenda sambamba na mitazamo ya watawala wanaopinga na kudunisha Afrika wa Ikulu ya Rais wa sasa wa Marekani.
Morocco ilikata uhusiano wake na Iran kwa madai kuwa harakati ya Hizbullah ya Lebanon inawasaidia wapigania uhuru wa Polisario huko Sahara Magharibi na kwamba ubalozi wa Iran nchini Algeria umesaidia mawasiliano baina ya Hizbullah na Polisario.