Rais Rouhani: Kutunza mazingira ni jukumu la kiutu, kijamii, kidini na kiutamaduni
Rais Hassan Rouhani amesema mchango wa dini una taathira katika kukuza utamaduni wa kutunza na kuhifadhi mazingira katika jamii za wanadamu.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameyasema hayo leo alipohutubia semina ya pili ya kimataifa ya mazingira, dini na utamaduni iliyofanyika hapa mjini Tehran kwa lengo la kustawisha mazungumzo baina ya tamaduni kwa ajili ya ustawi endelevu. Amesema mazingira yanaweza kuwa wenzo wa kuleta umoja baina ya wafuasi wa dini zote; na ili kuhifadhi mazingira hakuna njia nyengine ghairi ya kuwa na wastani katika mambo na kujiweka mbali na utumiaji mabavu na ubinafsi katika kuamiliana na maumbile.
Rais Rouhani amesisitiza kuwa kuyatunza mazingira ni jukumu muhimu la kiutu, kijamii, kidini na kiutamaduni kwa watu wote na kuongezea kwa kusema: utumiaji wa fueli za kisukuku na vita vya mtawalia vilivyotokea duniani hususan kuanzia karne ya 17 hadi 20 vimesababisha madhara makubwa kwa maumbile.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuwa ujumbe wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa dunia ni kuwa na kadiri na wastani katika mambo na kila mara inatangaza kwamba njia ya uokovu wa mwanadamu ni kuwa na wastani na kujiweka mbali na ufurutaji mpaka.../