Rouhani: Marekani imepoteza fursa ya kihistroria ya kusahihisha makosa yake
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema Marekani imepoteza fursa ya kipekee na ya kihistoria ya kusahihisha makosa yake kwa kukataa kulindolea taifa hili vikwazo haramu wakati huu ambapo Iran inakabiliana na ugonjwa wa Covid-19 unaosababishwana virusi vya corona.
Rais Hassan Rouhani alisema hayo jana Jumatano akizungumza kwenye kikao cha baraza la mawaziri mjini Tehran na kuongeza kuwa, "kwa bahati mbaya, Wamarekani hawajajifunza chochote hata katika kipindi hiki kigumu cha janga la kimataifa."
Amesema Marekani imekuwa ikichukua hatua zilizo dhidi ya taifa la Iran huku ikijificha ndani ngozi ya kondoo, lakini hii leo uhasama wao dhidi ya Wairani upo dhahiri na wazi zaidi kuliko wakati mwingine wowote ule.
Dakta Hassan Rouhani amesisitiza kuwa, vikwazo hivyo vya Marekani dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni batili, haramu na vya kikatili.
Amefafanua kwa kusema, utawala wa Marekani si tu umekataa kuliondolea taifa hili vikwazo haramu katika kipindi hiki cha mgogoro wa ugonjwa wa Covid-19, lakini umeenda mbali zaidi na hata kushadidisha vikwazo hivyo.
Rais wa Iran ameeleza bayana kuwa, licha ya kuwa taifa hili lipo chini ya vikwazo, lakini limefanikiwa pakubwa katika mapambano dhidi ya corona ikilinganishwa na nchi nyingi zilizostawi.