Iran yaonya kutoa jibu kali kwa chokochoko zozote za Marekani
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i64692-iran_yaonya_kutoa_jibu_kali_kwa_chokochoko_zozote_za_marekani
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imeonya kutoa jibu kali kwa chokochoko na hatua yoyote ya kiuadui itakayochukuliwa na serikali ya Marekani dhidi ya maslahi yake ya kitaifa.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Nov 18, 2020 04:07 UTC
  • Iran yaonya kutoa jibu kali kwa chokochoko zozote za Marekani

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imeonya kutoa jibu kali kwa chokochoko na hatua yoyote ya kiuadui itakayochukuliwa na serikali ya Marekani dhidi ya maslahi yake ya kitaifa.

Iran imetoa onyo hilo baada ya gazeti la New York Times la Marekani kuandika kuwa Rais Donald Trump wa Marekani imekuwa akifikiria kushambulia vituo vya nyuklia vya Iran.

Akiashiria suala hilo hapo jana Jumanne, Ali Rabiei, msemaji wa serikali ya Iran hata hivyo amesema kuwa anadhani suala hilo ni sehemu ya vita vya kisaikolojia vinavyoendeshwa na serikali ya Marekani na utawala haramu wa Israel dhidi ya Iran na kwamba kuna uwezekano mdogo kwa Marekani kutekeleza kivitendo hujuma kama hiyo ya kichokozi.

Inasemekana kuwa Trump alipendekeza fikra ya kushambuliwa vituo hivyo vya nyuklia vya Iran katika kikao na maafisa wake wa ngazi ya juu kijeshi hapo siku ya Alkhamisi, ambao walimuonya kwamba hujuma kama hiyo inaweza kusababisha mgogoro wa kieneo katika siku za mwisho za kuwa kwake ofisini.

Kituo cha nyuklia cha Iran, Bushehr

Viongozi wa Iran wamekuwa wakisisitiza kuwa mpango wao wa nyuklia ni wa malengo ya kiraia tu, jambo ambalo limethibitishwa na kusisitizwa mara kwa mara na Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Nyuklia IAEA.

Trump ambaye amekuwa akikosoa vikali mapatano ya kimataifa ya nyuklia kati ya Jamhuri ya Kiislamu na madola makuu ya dunia, yaliyotiwa saini mwaka 2015, aliiondoa nchi yake katika mapatano hayo May 2018 na kisha kuiwekea Iran vikwazo vya upande mmoja vinavyotajwa kuwa ni vya kulemaza na vikali zaidi kuwahi kuwekewa nchi yoyote ile ya dunia. Pamoja na hayo Iran imekuwa ikiendelea mbele na mradi wake wa nyuklia bila kutatizwa pakubwa na vikwazo hivyo wala mashinikizo ya juu kabisa ya Washington dhidi yake.