Mar 04, 2024 09:07 UTC
  • Ansarullah ya Yemen: Baada ya tuliyoizamisha, tutaendelea kuzishambulia meli za Uingereza katika Bahari Nyekundu

Yemen imeapa kuwa itaendelea kuzishambulia meli za Uingereza katika Bahari Nyekundu ili kuwaunga mkono Wapalestina katika Ukanda wa Ghaza, ambao wamekuwa wakiandamwa na vita vya mauaji ya kimbari vinavyoendeshwa na utawala wa Kizayuni wa Israel kwa muda wa miezi mitano sasa.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Yemen Hussein al-Ezzi ameyasema hayo katika ujumbe alioweka kwenye mtandao wa X, siku moja baada ya meli ya Uingereza iliyobeba makontena kuzama kwenye Bahari Nyekundu karibu wiki mbili baada ya kulengwa katika shambulio la kulipiza kisasi la Vikosi vya Ulinzi vya Yemen.
 
Ezzi ameeleza bayana: "Yemen itaendelea kuzamisha meli zaidi za Uingereza, na athari yoyote au hasara nyingine zote zitaongezwa kwenye bili ya Uingereza".
 
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Yemen ameongeza kuwa, ni utawala wa kijangili ndio unaoishambulia Yemen na washirika na Marekani katika kufadhili jinai zinazoendelea kufanywa dhidi ya raia huko Ghazza.
 
Meli kubwa ya kubeba mizigo ya M/V Rubymar inayomilikiwa na Kampuni ya Belize ya Uingereza, ilishambuliwa na jeshi la Yemen mnamo Februari 18 kwa makombora kadhaa ya majini katika Mlango-Bahari wa Bab al-Mandab, ambayo ni njia ya kimkakati ya majini inayounganisha Bahari Nyekundu na Ghuba ya Aden.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Yemen Hussein al-Ezzi 

Mamlaka za Yemeni zimeripoti kuwa meli ya Rubymar, ambayo ilikuwa imetelekezwa kwa siku 12, ilizama Ijumaa jioni wakati hali ya hewa ya dhoruba ilipotanda kwenye Bahari Nyekundu. Kamandi Kuu ya Majeshi ya Marekani (CENTCOM) ilitoa picha iliyoonyesha meli hiyo ikiwa imeelemea upande mmoja na kuthibitisha kuwa ilikuwa inazama.

Jeshi la Yemen limekuwa likizilenga meli za utawala wa Kizayuni Israel na zile zinazoelekea bandari za utawala huo haramu tangu mwezi Novemba mwaka jana kuonyesha mshikamano na Wapalestina wa Ghaza ambao kwa mwezi wa tano sasa wanaendelea kuandamwa na vita na mashambulio ya kinyama ya jeshi la Kizayuni ambayo hadi sasa yameshaua shahidi zaidi ya Wapalestina 30,320 wengi wao wakiwa wanawake na watoto na kujeruhi wengine 71,533.

Wayemen wametamka kinagaubaga kuwa hawatasita kufanya operesheni makini za kijeshi dhidi ya maslahi ya yeyote mwenye uadui na Yemen kwa ajili ya kulinda ardhi yao na kuthibitisha uungaji mkono wao usiotetereka kwa taifa la Palestina.../

Tags