Ripota wa UN: Israel ni mvamizi mbaya zaidi katika historia
Ripota maalumu wa Umoja wa Mataifa katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu amesema kuwa uvamizi wa Israel dhidi ya Palestina ulioanza zaidi ya miongo sita iliyopita ndio mbaya na machafu zaidi duniani.
Michael Lynk amesema tangu ilipovamia na kuikaliwa kwa mabavu ardhi ya Palestina Israel imekuwa ikighusubu haki za taifa hilo na kukanyaga sheria.
Amesema kuwa utawala ghasibu wa Israel pia unawakandamiza watu wa Palestina na wanaharakati wa kutetea haki za binadamu.
Michael Lynk ameashiria tangazo la Israel la kujenga nyumba 6,000 mpya za walowezi wa Kiyahudi katika maeneo ya Palestina sambamba na kiwango kikubwa cha uharibifu wa nyumba za Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi na Quds Mashariki (East Jerusalem) na ameituhumu Israel kuwa inadunisha ubinadamu wa Wapalestina. Vilevile amewasilisha ripoti yake dhidi ya Israel katika Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa.
Marekani, muitifaki mkuu wa utawala ghasibu wa Isrel, imepinga ripoti hiyo ya Umoja wa Mataifa na kutishia kuchukua hatua kali.