Waisrael washadidisha maandamano ya kumtaka Netanyahu ajiuzulu
Maelfu ya Waisraeli wamefanya maandamano katika mji mkuu Tel Aviv kushinikiza kujiuzulu Waziri Mkuu wa utawala ghasibu wa Israel, siku chache baada ya polisi ya Israel kupendekeza Benjami Netanyahu afunguliwe mashitaka kutokana na kashfa za ufisadi wa kifedha anazokabiliwa nazo.
Duru za habari zinasema, waandamanaji karibu elfu mbili walikusanyika jana Ijumaa katika Medani ya Tel Aviv, kushiriki maandamano hayo dhidi ya Netanyahu, wanayemtaja kuwa mfisadi wa kifedha.
Jumanne iliyopita, polisi ya Israel ilisema ina ushahidi wa kutosha wenye mashiko ya kumfunguliwa mashitaka ya ufisadi wa kifedha Netanyahu.
Uchunguzi wa maoni uliochapishwa Jumatano iliyopita unasema kuwa, karibu nusu ya wapiga kura huko Israel wanaiamini polisi, huku asilimia 25 pekee wakiwa na imani na Waziri Mkuu huyo, huku asilimia 26 wakisema hawajui ni nani wa kuamini kwenye kashfa za ufisadi zinazomzunguka Netanyahu.
Maandamano ya kutaka kumuondoa madarakani Netanyahu na kuharakishwa uchunguzi dhidi yake yalianza miezi kadhaa iliyopita mjini Tel Aviv na katika maeneo mengine ya Palestina inayokaliwa kwa mabavu.