Baraza Kuu la Kisiasa la Yemen lateua wajumbe wake wapya
Mahdi al Mashat amewateuwa wajumbe 32 wapya wa Baraza Kuu la Kisiasa la Yemen katika hatua yake ya kwanza kama mkuu mpya wa baraza hilo.
Mahdi al Mashat ameteuliwa kuwa Mkuu Mpya wa Baraza Kuu la Kisiasa la Yemen kufuatia kuuliwa Saleh al Sammad mwenyekiti wa zamani wa baraza hilo; na tayari amekula kiapo mbele ya wabunge wa Yemen.
Saleh al Sammad aliyekuwa Mkuu wa Baraza Kuu la Kisiasa la Yemen aliuawa shahidi Alhamisi iliyopita katika shambulio la ndege za kivita za muungano vamizi unaoongozwa na Saudia katika mkoa wa al Hudaidah magharibi mwa Yemen.

Habari nyingine inasema kuwa jeshi na kamati za kujitolea za wananchi wa Yemen zimeanza kutekeleza oparesheni kubwa dhidi ya mamluki wa Saudi Arabia katika mikoa ya Lahij kusini mwa Yemen na huko Taiz kusini magharibi mwa nchi hiyo. Wakati huo huo ndege za kivita za muungano vamizi unaoongozwa na Saudi Arabia zimelishambulia mara mbili tawi moja la Benki Kuu katika mkoa wa Saada kaskazini mwa Yemen. Wanajeshi wa Yemen pia wamekishambulia kituo cha kijeshi cha al Sadis huko Najran kusini mwa Saudia na kuisambaratisha gari moja ya jeshi.