Mataifa ya Kiislamu yaandamana kupinga US kuuhamishia ubalozi wake Quds
Maelfu ya watu wameshiriki maandamano ya kupinga hatua ya kiuhasama ya Marekani ya kuuhamishia ubalozi wake katika mji wa Quds Tukufu, kutoka Tel Aviv.
Karibu watu 7,000 walishiriki maandamano hayo baada ya Sala ya Ijumaa hapo jana katika eneo la Bonde la Jordan nchini Jordan huku waandamanaji hao wakitangaza uungaji mkono wao kwa Wapalestina.
Kadhalika watu 5,000 walishiriki maandamano hayo katika mji mkuu wa Indonesia, Jakarta na maelfu ya wengine katika mji wa Istanbul nchini Uturuki, wote wakipiga nara za kulaani chokochoko hizo za Marekani huku wakiwa wamebeba bendera ya Palestina.
Licha ya upinzani kutoka kila kona ya dunia, lakini Rais Donald Trump wa Marekani ametangaza kuwa, wiki ijayo serikali ya Washington itafungua ubalozi wake katika mji wa Quds unaokaliwa kwa mabavu na utawala ghasibu wa Israel.
Disemba 6 mwaka jana Trump alitangaza hatua hiyo ambayo ni kinyume na maazimio ya kimataifa ya kuitangaza Quds Tukufu kuwa eti mji mkuu wa utawala haramu wa Israel.
Uamuzi huo wa Trump ulipelekea kuibuka wimbi kubwa la malalamiko huko Palestina na kufuatiwa na maandamano yanayojulikana kama "Haki ya Kurejea" ambayo yalianza tangu Machi 30 mwaka huu, na yanatazamiwa kuwa makubwa zaidi siku hiyo ambayo Marekani imetangaza kuuhamishia ubaliozi wake Baitul Muqaddas.