Wanamuqawama wa Palestina wasitisha vita baada ya Israel kukubali masharti yao
Baada ya utawala haramu wa Kizayuni kukubali masharti ya wanamuqawama wa Palestina, makundi ya Kipalestina ikiwemo Harakati ya Jihadul-Islami yamekubali pendekezo la Misri kwa ajili ya kusimamisha vita.
Kiongozi mmoja wa Harakati ya Jihadul-Islami amesema kuwa kufuatia utawala huo haramu kukubali masharti ya makundi ya Kipalestina kuhusiana na kuacha kuwaua kigaidi viongozi wa muqawamana na kuacha kuwapiga risasi Wapalestina wanaoandamana katika wimbi la maandamano ya haki ya kurejea, nayo makundi ya Kipalestina yamesitisha mapigano dhidi ya utawala huo. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, usitishaji vita huo umeanza kutekelezwa leo asubuhi. Jana usiku Ziyad al-Nakhalah, Katibu Mkuu wa Harakati ya Jihadul-Islami alinukuliwa akisema kuwa, Wazayuni ndio walioomba usitishaji sambamba na kutangaza kukubali masharti ya wanamuqawama. Inafaa kuashiria kuwa, utawala huo katili ulianzisha mashambulizi yake ya kinyama Jumanne asubuhi ambayo yamesababisha makumi ya watu kuuawa. Wakati huo huo watu sita wa familia moja wameripotiwa kuuawa katika shambulizi la ndege za utawala haramu wa Israel katika eneo la Deir al Balah, katikati mwa Ukanda wa Gaza, shambulizi lililotekelezwa mapema leo asubuhi.

Katika hujuma hiyo ya kinyama watu wengine 12 wamejeruhiwa. Taarifa iliyotangazwa na idara ya afya ya eneo la Ukanda wa Gaza, imesema kwa akali watu 32 akiwemo Baha Abu al-Ata, kamanda wa Kikosi cha al-Quds Tawi la Harakati ya Jihadul-Islami, aliyekuwa na umri wa miaka 42 wameuawa katika hujuma hizo za jinai huku watu wengine 100 wakijeruhiwa. Nchi nyingi pamoja na asasi mbalimbali za kimataifa zimelaani vikali mashambulizi hayo ya kinyama ya utawala huo pandikizi wa Kizayuni. Katika kujibu hujuma hizo wanamuqawama wa Palestina wamefyatua mamia ya makombora na marokei kuelekea vitongoji vya walowezi wa Kizayuni ukiwemo mji mkuu wa Israel, Tel Aviv na kusababisha hasara kubwa ya roho na mali.