Msemaji wa Hamas: njia pekee ya kuwafukuza Wazayuni ni muqawama
Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) amesema kuwa njia pekee ya kuwarejsha nyuma Wazayuni ni kuendeleza mapambano na kuongeza kuwa: Maandamano yanayofanywa na wananchi wa Palestina katika maeneo mbalimbali yametuma ujumbe kwamba wataendeleza muqawama na mapambano hadi kupatikane ushindi.
Hazim Qassim ameeleza kuwa maghasibu wanadhani kuwa wanaweza kudhibiti ardhi zaidi za Wapalestina bila ya Wapalestina kuendesha muqawama wowote, katika hali ambayo mipango yote hiyo itafuatiliwa na muqawama wa wananchi wa Palestina.
Hazim Qassim amesema kuwa Donald Trump na Benjamin Netanyahu wanakiuka sheria za kimataifa na kuongeza kuwa hii leo tunashuhudiwa kutengwa Marekani na jamii ya kimataifa kutokana na hatua yake ya kuwaunga mkono na kuwasaidia Wazayuni.
Msemaji wa Hamas ameitaja serikali ya Marekani kuwa nembo ya ubeberu duniani.
Harakati ya Jihad Islami ya Palestina pia huko pamoja na Hamas zilikuwa tayaeri zimetoa taarifa zikisisitiza kuwa ziko tayari kukabiliana na chokochoko za utawala wa Kizayuni wa Israel.
Utawala wa Kizayuni ulipanga kuanzia jana Julai Mosi kuyatwaa maeneo ya Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na kuyaunganisha na ardhi zilizoghusubiwa za Palestina.