WFP: Wayemen milioni 10 wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula
Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) limesema wananchi milioni 10 wa Yemen wanaandamwa na ubaha mkubwa wa chakula.
Shirika hilo la Umoja wa Mataifa limesema linahitaji dola milioni 737 kufikia mwishoni mwa mwaka huu, ili kukabiliana na baa la njaa linaloisumbua nchi hiyo ya Kiarabu.
Elisabeth Byrs, msemaji wa WFP amesema hayo katika mkutano uliofanyika mjini Geneva na kuongeza kuwa, mgogoro wa kibinadamu nchini humo upo katika hali ya kutisha.
Amesema dunia inapaswa kuchukua hatua za dharura haraka iwezekanavyo na kwamba hatari ya njaa inaikabili zaidi ya asilimia 80 ya watu wote wa jamii ya nchi hiyo.
Yemen ilivamiwa na kushambuliwa na Saudi Arabia na washirika wake wanaosaidiwa na Marekani, Israel na nchi nyingine za Magharibi hapo mwaka 2015 na inaendelea kuzingirwa baharini, nchi kavu na angani.
Mashambulizi hayo ya Saudia na washirika wake yameua maelfu ya raia wasio na hatia na kuwalazimisha mamilioni ya wengine kuwa makimbizi.