Mufti wa kundi la kigaidi la Daesh atiwa mbaroni Kirkuk, Iraq
Vikosi vya usalama vya Iraq vimemtia mbaroni Mufti wa kundi la kigaidi na la ukufurishaji la Daesh (ISIS) katika mkoa wa Kirkuk kaskazini mwa nchi hiyo.
Bila kuashiria jina la gaidi huyo wa Daesh aliyetiwa mbaroni, duru za habari za Iraq jana Jumatano zilitangaza kuwa, gaidi huyo ni mufti wa ofisi iitwayo "Kitengo cha Haki na Malalamiko cha al Abbasi." Kwa mujibu wa ripoti hiyo, gaidi huyo alitiwa mbaroni katika eneo la al Haria kufuatia msako uliofanywa na Idara ya Intelijinsia ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Iraq kwa kusaidiana na vyombo vya habari.
Jumamosi iliyopita pia magaidi wa Daesh 24 walitiwa mbaroni katika oparesheni ya kiintelijinsia iliyofanywa na askari wa Iraq mkoani Nainawa kaskazini mwa Iraq. Mikoa ya Kirkuk, Nainawa, Al Anbar, Diyala na Salahuddin huko kaskazini na magharibi mwa Iraq ni vituo vikuu vya masalia ya magaidi wa kundi la Daesh.
Jeshi la Iraq limekuwa likiendesha operesheni dhidi ya masalia na mamluki wa kundi la kigaidi la Daesh hususan katika maeneo ya mikoa ya Kirkuk, Salahuddin na Diyala maarufu kwa jina la " Pembe Tatu za Mauti."