Marekani yaingiza shehena ya zana za kijeshi mashariki mwa Syria
Duru mbalimbali za habari zimearifu kuwa, silaha na zana za kilojistiki za wanajaeshi magaidi wa Marekani zimeonekana zikiingizwa katika maidani ya mafuta huko Koniko kaskazini mashariki mwa Deir Zor.
Shirika la habari la Syria, SANA limeripoti kuwa msafara wa wanajeshi wa Marekani jana Jumatatu uliwasili katika maidani ya mafuta vya Koniko kaskazini mashariki mwa mkoa wa Deir Zor. Msafara huo wa wanajeshi wa Marekani ulikuwa umejizatiti kwa silaha na zana za kilojistiki.
Marekani imetuma zana hizo za kijeshi huko Deir Zor kwa lengo la kuimarisha uwepo wa wanajeshi wake kinyume cha sheria maidani hiyo ya mafuta ya Syria na kuendelea kupora maliasili hiyo ya mafuta.
Marekani siku zote inatuma silaha na zana za kilojistiki katika maeneo inayoyakalia kwa mabavu na katika kambi zake za kijeshi ilizoasisi kaskazini mwa Syria kinyume cha sheria. Ni wazi kuwa, Marekani imegeuza maidani ya mafuta, shule na hospitali zilizoko katika maeneo ya mashariki mwa Syria ukiwemo mkoa wa Deir Zor kama kambi zake za kijeshi.
Katika siku na miezi ya karibuni wanajeshi wa Marekani waliingiza mamia ya magari yao katika mkoa wa Hasakah kupitia vivuko haramu ili kutumika katika kambi zake za kijeshi na kuyasaidia pia makundi ya kigaidi na taasisi zake vibaraka.