Wanajeshi vamizi wa Marekani wanapora ngano ya Syria
Wanajeshi vamizi wa Marekani wamepora malori 38 ya ngano ya Syria iliyokuwa katika maghala huko Tal Alou katika mkoa wa Hasaka kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Shirika la Habari la Syria SANA limesema jeshi la Marekani limepora malori 38 ya ngano ya Tal Alou na kuipeleka Iraq kupitia kivuko cha mpakani cha Al Walid.
Hayo yanajiri wakati ambao Waziri wa Mafuta wa Syria Bassam Tomeh hivi karibuni alitangaza kuwa wanajeshi vamizi wa Marekani na magaidi wakufurishaji wamekuwa wakipora mafuta ya petroli ya nchi hiyo ya Kiarabu.
Hivi sasa Marekani inakalia kwa mabavu asilimi 90 ya visima vya mafuta katika eneo la kaskazini mashariki mwa Syria.
Amesema vita vimesababisha sekta ya mafuta ya Syria kupata hasara ya moja kwa moja na isiyo ya moja kwa moja ya dola bilioni 92.
Tokea mwaka 2019, Marekani iliingiza wanajeshi wake katika maeneo ya visima vya mafuta vilivyo katika mikoa ya Al Hasakah na Deir ez-Zor ambayo inadhibitiwa na Wakurdi kaskazini mashariki mwa Syria.
Kamandi ya Wanajeshi wa Marekani katika eneo la Asia Magharibi iliwahi kutangaza kuwa, wanajeshi wa Marekani watabakia nchini Syria kwa ajili ya kupora utajiri wa mafuta ya nchi hiyo.
Serikali ya Syria inasisitiza kuwa, uwepo wa wanajeshi wa Marekani na waitifaki wake nchini humo ni sawa na kuikalia kwa mabavu nchi hiyo.