Wasiwasi kuhusu hatima ya watoto wakimbizi elfu 9 huko Ujerumani
Polisi ya Ujerumani imetangaza kuwa karibu watoto wakimbizi elfu tisa nchini humo wametoweka, hatua ambayo imezidisha hali ya wasiwasi kuhusu uwezekano wa watoto hao kuuzwa na kutumiwa vibaya na magenge ya biashara haramu ya binadamu katika nchi za Ulaya.
Kitengo cha polisi ya upelelezi ya Ujerumani kimetangaza kuwa viongozi wa nchi hiyo hawana taarifa yoyote kuhusu watoto elfu nane na 991 waliosajiliwa nchini humo kama wakimbizi. Watoto 867 kati ya idadi hiyo iliyotajwa wana umri wa miaka 13 au chini ya hapo; huku wengi wao wakiwa na umri kati ya miaka 14 hadi 17.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, polisi ya Ujerumani imeongeza kuwa idadi ya watoto na mabarobaro waliotoweka nchini humo imeongezeka mara mbili tangu kuanza mwaka huu wa 2016 hadi hivi sasa. Kuna wasiwasi huu kuwa makundi ya magendo ya binadamu huenda yakawatumia vibaya watoto hao wakimbizi. Taasisi za kuwalinda Watoto zimebainisha hatari iliyopo iwapo watoto hao wakimbizi waliotoweka huko Ujerumani watatumiwa vibaya na magenge yaliyotajwa.
Wakati huo huo Shirika la Save the Children limetangaza kuwa limepata wasiwasi mkubwa kufuatia takwimu hizo mpya zilizotolewa na polisi ya Ujerumani. Ripoti hiyo imetolewa zikiwa zimepita wiki kadhaa tu baada ya kundi hilo kusema kuwa lina uthibitisho unaoonyesha kuwa idadi kadhaa ya watoto wakimbizi wamelazimika kufanya kazi kwa lazima huko Italia.