Maandamano dhidi ya ubaguzi wa Trump yapamba moto US
Maelfu ya watu pasina kujali dini na rangi zao wameshadidisha maandamano katika kona mbali mbali za Marekani, kulaani sheria tata ya ubaguzi iliyopasishwa na Rais Donald Trump wa nchi hiyo hivi karibuni.
Maandamano hayo yamepamba mto katika maeneo ya Minneapolis, Minnesota, Massachusetts, New York, South Carolina Columbia na Virginia, huku waandamanaji wakibebe mabango yenye jumbe za kukosoa ubaguzi wa Trump. Baadhi ya mabango hayo yalikuwa na maneno yanayosema, "Wakimbizi karibuni, mnakarabishwa hapa."
Betsy Hodges, Meya wa Minnepolis ambaye jana Jumanne aliungana na waandamanaji hao alisema: "Tutasimamia haki, Trump anajaribu kuiadhibu miji inayoshuhudia maandamano dhidi ya serikali yake, kwa kupunguza pesa za hazina za miji. Hilo halitubabaishi."
Naye Jaylani Hussein, Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Mahusiano ya Kiislamu Marekani CAIR tawi la Minnesota ambaye pia alishiriki maandamano amesema kuwa, taasisi hiyo pamoja na mashirika mengine ya kutetea haki za Waislamu nchini Marekani yatafungua kesi dhidi ya utawala wa kibaguzi wa Trump kutokana na ubaguzi wake.
Kamishna wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa, Zeid Ra’ad Zeid al-Hussein amesema kuwa ni marufuku na kinyume cha sheria kuwabagua watu kwa mujibu wa utaifa wao, na kwamba sheria ya kuwazuia Waislamu kuingia nchini Marekani iliyoanza kutekelezwa Marekani ni ya kikatili na sababu ya kuharibiwa rasilimali zinazohitajika kwa ajili ya kupambana ipasavyo na ugaidi.
Mbali na Umoja wa Mataifa, mashirika ya kutetea haki za binadamu ya Human Rights Watch na Amnesty International na serikali za nchi zilizopigwa marufuku pia zimekosoa vikali sheria hiyo ya kibaguzi ya Trump, ya kuzuia wakimbizi na raia wa nchi saba za Kiislamu ikiwemo Iran kuingia nchini humo.