WFP yaomba msaada kuokoa maisha ya maelfu ya watoto Afrika, Yemen
Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula Duniani WFP limetoa wito wa msaada wa Umoja wa Ulaya ili kuokoa maisha ya mamia ya maelfu ya watoto wa Afrika na Yemen wanaokabliwa na baa la njaa.
Mkurugenzi wa WFP David Beasley akizungumza Jumatatu ametoa wito kwa Umoja wa Ulaya kutoa mchango wa dola bilioni moja katika kipindi cha miezi michache ijayo kuokoa maisha ya mamia ya maelfu ya watoto wa Afrika na Yemen wanaokabiliwa na hatari ya kupoteza maisha kutokana na njaa.
Amesema hivi sasa watu milioni 20 nchini Yemen wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula katika nchi za Yemen, Sudan Kusini, Somalia na Nigeria. Ameongeza kuwa nchi hizo zinakabiliwa na maafa makubwa zaidi ya kibinadamu kuwahi kushuhudiwa duniani tokea mwaka 1945.
Mkuu wa WFP anasema iwapo misaada haitafika haraka, kuna uwezekano wa watoto 600,000 kupoteza maisha kutokana na ukosefu wa chakula katika nchi zote nne ambazo zinakabiliwa na vita.
Tokea Machi 2015 Yemen imekuwa ikikabiliwa na hujuma ya kila siku ya Saudi Arabia na waitifaki wake. Huko Sudan Kusini kuna vita vya ndani vilkivyoanza mwaka 2013 huku Nigeria nayo ikikabiliwa na hujuma ya kundi la magaidi wakufurishaji wa Boko Haram waliopelekea idadi kubwa ya watu, wakiwemo wakulima kukimbia makazi yao kaskazini mwa nchi hiyo. Nchini Somalia nako pia tokea mwaka 1992 kumekuwa na vita vya ndani huku miaka ya hivi karibni ikishuhudia kushadidi hujuma za magaidi wakufurishaji wa Al Shabab.