Waziri Mkuu wa Pakistan ajiuzulu kufuatia uamuzi wa mahakama
Waziri Mkuu wa Pakistan, Nawaz Sharif amejiuzulu wadhifa wake baada ya Mahakama ya Juu nchini humo kumuengua madarakani kutokana na kashfa ya ufisadi.
Akisoma hukumu dhidi yake hii leo, Jaji Ejaz Afzal Khan wa mahakama hiyo amesema Nawaz Sharif amevuliwa ubunge na kwa msingi huo amepoteza wadhifa wake wa Uwaziri Mkuu wa nchi hiyo.
Uamuzi wa Mahakama ya Juu ya Pakistan umetolewa baada ya kubainika kuwa, Sharif pamoja na familia yake walikuwa miongoni mwa shakhsia walioficha fedha za umma nje ya nchi kwa maslahi yao binafsi.
Ufichuzi huo uliwekwa hadharani kwa mara ya kwanza na nyaraka za siri zilizofichuka hivi karibuni zijulikanazo kama 'Nyaraka za Panama'.
Majaji watano wa Mahakama ya Juu katika mju mkuu Islamabad wamesema baada ya kusikiliza kwa makini na kuangalia ushahidi uliokuwa mbele yao, wamebaini kuwa ni kweli Sharif alihusika na hivyo amekosa uaminifu kwa wananchi wa taifa hilo.
Mbali na Waziri Mkuu, Mahakama ya Juu ya Pakistan pia imetengeua uteuzi wa Ishaq Dar, Waziri wa Fedha wa nchi hiyo, ambaye alikuwa mpambe wa karibu wa Nawaz Sharif.