UNHCR: Waislamu Warohingya wa Myanmar wanahitajia misaada ya kibinadamu
Kamishna Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR amesema kuwa, Waislamu wa jamii ya Rohingya wa nchini Myanmar wanahitajia misaada ya kibinadamu na kwamba, Waislamu hao wamevumilia mateso na madhara mengi ya kisaikolojia.
Filippo Grandi amesema kuwa, msaada muhimu na wa haraka wanaohitajia Waislamu hao ni kupata sehemu mwafaka ya kukaa. Kamishna Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR ameongeza kuwa, kabla ya Waislamu Warohingya kuwa wakimbizi walikumbwa na matatizo na madhara mengi ya kimwili huku kundi jingile likiathirika na kukumbwa na matatizo ya kisaiokolojia.
Kamishna Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR ameashiria dhulma na ukatili mwingi uliofanywa dhidi ya Waislamu wa Kirohingya wa nchini Myanmar na kubainisha kwamba, kuna haja kwa Waislamu hao kuungwa mkono kimataifa.
Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Stephane Dujarric amesema Shirika la Kuhuhudumia Wakimbizi la Umoja huo limezidisha operesheni za kupelekea misaada ya kibinadamu hususan mablanketi kwa wakimbizi wa Myanmar huko Bangladesh ili kuwakinga na matatizo yanayosababishwa na mvua na upepo.
Maelfu ya Waislamu wa jamii ya Rohingya wameuawa katika mashambulizi yanayoendelea kufanywa na Jeshi la Myanmar na Mabudha wenye misimamo ya kuchupa mipaka hususan katika jimbo la Rakhine.
Wimbi jipya la mauaji ya Waislamu wa Rohingya katika jimbo hilo lililoko magharibi mwa Myanmar lilianza tarehe 25 Agosti mwaka huu.