Oct 21, 2017 16:24 UTC
  • Maulama wa Suni na Shia Lebanon wasisitizia mapambano dhidi ya ugaidi

Maulama wa Kiislamu wa madhehebu za Shia na Suni nchini Lebanon wanesema kuwa kufeli mradi kabambe wa Marekani na Israel kupitia ugaidi, hakuna maana ya kumalizika kwa vita na wametoa wito wa kuendelezwa muqawama kwa ajili ya vita vya baadaye.

Hayo yameelezwa na maulama hao katika kikao cha wiki moja kilichomalizika Ijumaa ya jana na kusisitiza kuwa, eneo la Mashariki ya Kati hivi sasa linashuhudia saa za mwisho za uhai wa kundi la kigaidi na ukufurishaji la Daesh (ISIS) na kusambaratika kwa njama za Israel na Marekani.

Magaidi wa Kiwahabi wanaotekelekeza mradi wa Marekani na Israel

Wasomi hao wa Kiislamu wamesisitiza kuwa, mapambano yamepata ushindi na kwamba muda si mrefu kutatolewa tangazo la mwisho la ushindi nchini Iraq na Syria.

Kikao hicho cha maulama wa Kiislamu kimebainisha kwamba, kushindwa mradi wa Wazayuni na Marekani (yaani ugaidi) hakuna maana ya kumalizika kwa vita, kwa sababu vita bado vinaendelea na kwamba kumalizika vita hivyo ni mwanzo wa vita nyingine katika medani nyingine ya mapambano. Wamefafanua kwamba kwa msingi huo muqawama unatakiwa kujiweka tayari kwa ajili ya kukabiliana na njama mpya za adui.

Wanamuqawama wa Hizbullah wanaoshiriki kuwaangamiza magaidi wa Kiwahabi

Kadhalika maulama hao wa Kishia na Kisuni nchini Lebanon wamepongeza msimamo wa kishujaa wa Marzouq Al-Ghanim, Spika wa Bunge la Kuwait katika kikao cha Jumuiya ya Kimataifa ya Mabunge ya Dunia huko Saint Petersburg, Russia, aliyesimama kidete na kuukemea vikali ujumbe wa bunge la utawala wa Kizayuni wa Israel na kuulazimisha kuondoka katika mkutano huo wa kimataifa. Katika kikao hicho al-Ghanim aliwataja wabunge wa Israel kuwa ni watu wasio na aibu na kuwataka waondoke katika ukumbi wa mkutano huo mara moja. Alisema: "Iwapo mna chembe ya heshima, nyinyi maghasibu na wauaji watoto ondokeni."

Tags