Mahakama Kuu Uhispania: Ole wake Carles Puigdemont asipohudhuria kotini
Mahakama Kuu ya Uhispania imemuonya rais wa eneo la Catalonia, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo aliyeuzuliwa madarakani kwa kutohudhuria mahakamani.
Jana Alkhamisi mahakama hiyo ilitoa onyo kwamba, ikiwa Carles Puigdemont, aliyevuliwa na serikali kuu ya Madrid madaraka ya urais wa Catalonia hatofika mahakamani kujieleza juu ya kuhusika na tangazo la kujitenga eneo hilo, basi mahakama hiyo itatoa hukumu ya kutiwa mbaroni.
Carles Puigdemont ambaye kwa sasa anadhaniwa kuwa yuko mjini Brussels, Ubelgiji pamoja na shakhsia wengine 13 waliovuliwa madaraka na serikali ya ndani ya Catalonia, anatuhumiwa kwa uasi, kuzusha fitina au usimamzi mbaya wa mali ya umma. Hata hivyo Puigdemont sambamba na kukanusha tuhuma dhidi yake amesema kuwa, tuhuma hizo zina msukumo wa kisiasa.
Hii ni katika hali ambayo baadhi ya viongozi waliouzuliwa wa eneo la Catalonia Alkhamisi ya jana walifika mahakamani kutoa maelezo yao juu ya namna walivyohusika katika sakata hilo. Kabla ya hapo Mariano Rajoy, Waziri Mkuu wa Uhispania alitangaza kuvunja bunge la Catalonia kuzingatia hatua ya upande mmoja ya bunge la eneo hilo kutangaza kujitenga na serikali kuu ya Madrid.