UN: Vifo vya raia Afghanistan vimevunja rekodi
Umoja wa Mataifa umetoa takwimu zinazoonyesha kuwa idadi ya vifo vya raia katika mgogoro uliodumu kwa muda mrefu nchini Afghanistan vimevunja rekodi kwa kuwa na watu 1,692 waliouawa katika miezi sita ya kwanza ya mwaka huu wa 2018.
Ujumbe wa Usaidizi wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan (UNAMA) umesema katika ripoti iliyochapishwa leo kuwa idadi ya vifo vimeongezeka kwa asilimia moja zaidi ikilinganishwa na mapema mwaka jana. Mashambulizi ya makundi ya wanamgambo na milipuko ya mabomu vimetajwa kuwa vyanzo vikuu vya vifo vya raia katika nchi hiyo iliyoathiriwa na vita.
Ripoti ya UNAMA imeeleza pia kwamba, raia wengine 3,430 wa Kiafghani wamejeruhiwa; kiwango ambacho kimetajwa kuwa cha chini kwa asilimia tano kulinganisha na idadi ya majeruhi wa mwaka uliopita. Ujumbe huo wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan umeongeza kuwa raia hao wameuawa nchini humo licha ya kuwepo makubaliano ya usitishaji vita ya aina yake yaliyofikiwa kati ya vikosi vya usalama na wanamgambo wa Taliban mwezi uliopita.