Russia yaionya Marekani isicheze na moto Syria
Waziri wa Mambo ya Nje wa Russia ameionya Marekani isicheze na moto huko Syria kwa kuchochea hujuma bandia ya silaha za kemikali ili kuhalalisha shambulizi dhidi ya wanajeshi wa Syria
Sergei Lavrov kwa mara nyingine ametahadharisha kuwa, kuna mpango wa kufanywa shambulizi bandia la silaha za kemikali katika mkoa wa Idlib nchini Syria ili kutoa mwanya kwa vikosi vinavyoongozwa na Marekani kushambulia wanajeshi wa Syria walio katika oparesheni dhidi ya magaidi eneo hilo. Akizungumza mjini Moscow akiwa ameandamana an mwenzake wa Syria Walid Muallem, Lavrov amesema nchi za Magharibi ndizo zinazopanga shambulizi hilo bandia la silaha za kemikali ili kuzuia operesheni dhidi ya magaidi huko Idlib ambayo ndiyo ngome yao ya mwisho nchini Syria. Amesema Russia ina ushahidi kuhusu njama hizo na imeshatoa tahadahri kwa nchi za Magharibi.
Hii si mara ya kwanza kwa nchi za Magharibi kufanya hujuma bandia za silaha za kemikali nchini Syria ili kuilaimu serikali ya nchi hiyo na hatimaye kuhalalsiha mashambulizi yenye lengo la kudhoofisha uwezo wa kijeshi wa Damascus. Mwezi Aprili mwaka huu pia kulifanywa hujuma bandia ya silaha za kemikali katika mji wa Douma nchini Syria na baadaye kudai kuwa eti Damascus ndiyo iliyofanya shambulizi hilo na hivyo kuhalalisha mashambulizi ya Marekani, Ufaransa na Uingereza dhidi ya Syria.