Mbunge wa Uturuki aionya Marekani juu ya kuishambulia kijeshi Iran
Öztürk Yılmaz, mbunge wa Uturuki, ameionya Marekani juu ya kuchukua hatua yoyote ya kijeshi dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inayoweza kuibua mapigano katika eneo.
Yılmaz ambaye ni mwanadiplomasia na mwanasiasa mashuhuri nchini Uturuki amebainisha kwamba mapigano yoyote madogo ya kijeshi kati ya Marekani na Iran, yanaweza kuibua vita vikubwa katika eneo hili ambavyo Rais Donald Trump kamwe hatoweza kuvizima. Mbunge huyo wa Uturuki sambamba na kukosoa kuendelea vikwazo vya upande mmoja vya Marekani dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, vikwazo hivyo vina taathira hasi pia kwa uchumi wa Uturuki.
Hii ni katika hali ambayo mara zote Iran imekuwa ikisisitiza kwamba Washington ni lazima ihitimishe mzozo wa kijeshi, vita na ugaidi wake wa kiuchumi dhidi ya watu wa taifa hili. Tarehe 8 Mei mwaka jana Trump alichukua hatua ya upande mmoja sambamba na kukiuka ahadi za Washington katika mapatano ya kimataifa ya nyuklia ya JCPOA na kuiondoa nchi yake katika mapatano hayo. Kufuatia hatua hiyo, Trump alirejesha tena vikwazo vya nyuklia dhidi ya Tehran, hatua ambayo ililaaniwa vikali ndani na nje ya Marekani.