Korea Kaskazini: Marekani haina kitu kipya cha kuwasilisha kwenye mazungumzo
(last modified Fri, 13 Dec 2019 15:10:57 GMT )
Dec 13, 2019 15:10 UTC
  • Korea Kaskazini: Marekani haina kitu kipya cha kuwasilisha kwenye mazungumzo

Wizara ya Mambo ya Nje ya Korea Kaskazini imesema kuwa, Marekani haina kitu kipya inachoweza kukiwasilisha kwenye mazungumzo na serikali ya Pyongyang.

Shirika rasmi la habari la Korea Kaskazini (KCNA) limeinukuu Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo ikisema kuwa, hata kama serikali ya Pyongyang itaanzisha tena mazungumzo na Washington, bado Marekani itakuwa haina kitu chochote cha maana cha kuwasilisha kwenye meza ya mazungumzo, kama ambavyo pia haina ukweli wowote. Ikiashiria msimamo wa hivi karibuni wa Marekani kuihusu serikali ya Pyongyang katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Wizara ya Mambo ya Nje ya Korea Kaskazini imesisitiza kuwa, nchi hiyo haina kitu cha kupoteza kama ambavyo imejiandaa kutoa jibu kali kwa hatua yoyote mkabala itakayochukuliwa na Washington dhidi yake.

Viongozi wa Marekani na Korea Kaskazini 

Hadi sasa Rais Donald Trump wa Marekani na Kim Jong-un, Kiongozi wa Korea Kaskazini wameshafanya duru tatu za mazungumzo nchini Singapore, Vietnam na katika mpaka wa Korea mbili. Hata hivyo mazungumzo hayo yalivunjika kutokana na kupenda makubwa kwa Marekani na kushindwa kwake kutekeleza ahadi ilizozitoa kwa ajili ya Korea Kaskazini. Aidha serikali ya Pyongyang inapinga uwepo kijeshi wa Marekani katika Rasi ya Korea ambapo katika uwanja huo iliipatia Washington muhula hadi mwishoni mwa mwaka huu, ihakikishe kuwa imerudi kwenye meza ya mazungumzo na kuiondolea vikwazo na kinyume na hivyo basi ijiandae kukumbwa na hatima mbaya.

Tags