Marekani yafanya "uharamia" wa kuiba maski za Wajerumani zilizokuwa zinatokea China
Ujerumani imeituhumu Marekani kuwa imetumia mbinu za uharamia katika kupora maski zake za kukabiliana na ugonjwa wa corona.
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Ujerumani Andreas Geisel amesema hatua ya Marekani kupora maski hizo za uso ni ‘uharamia wa kisasa’.
Vyombo vya habari vya Ujerumani vimeripoti kuwa maelfu ya maski ambazo zilikuwa zimenunuliwa kutoka shirika la 3M zimeelekezwa Marekani wakati zilipokuwa zikihamishwa baina ya ndege nchini Thailand zikitokea China.
Wakuu wa Ujerumani wamethibitisha kuwa maski 200,000 aina ya FFP2- ambazo zinashabihiana na zile za N95 zinazotumiwa Marekani, ziliibiwa katika uwanja wa ndege wa Bangkok na hivyo hazikufika Berlin. Ujerumani imesema tayari ilikuwa imeshalipia maski hizo ambazo zimeibiwa na maajenti wa Marekani nchini Thailand.
Akiwa ni mwenye hasiria, Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani alisema siku ya Ijumaa kuwa, ‘Hii sio njia ya kuamiliana baina ya washirika wa Atlantiki.” Ameongeza kuwa hata kama kuna mgogoro wa kimataifa hakupaswi kutumiwa mbinu za magenge ya zamani ya Kimarekani. Waziri huyo amesema serikali ya Ujerumani itawasilisha malalamiko rasmi na kuitaka Marekani iheshimu sheria za kimataifa.
Ubalozi wa Marekani mjini Berlin, Ujerumani bado haujatoa taarifa kuhusu tukio hilo la uhalifu wa kimataifa.
Taarifa zaidi zinasema shirika la kijasusi la Israel, Mossad linateleza oparesheni maalumu za kimataifa za kupora vifaa vya kukabiliana na corona na kuvipeleka Israel.
Mwezi uliopita maafisa wa forodha wa Ujerumani walitangaza kuwa maski milioni 6 zilizoagizwa kwa ajili ya kuwalinda wafanyakazi wa afya walio mstari wa mbele wa vita dhidi ya corona zilipotea kwenye uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta mjini Nairobi, Kenya.Taarifa hiyo iliyochapishwa na gazeti la Spiegel Online ilisema "Mamlaka zinajaribu kufahamu kilichotokea." Msemaji wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege vya Kenya (KAA) alisema upelelezi bado haujapata chochote hadi sasa.