Matumaini baada ya watafiti kugundua dawa ya kutibu corona
https://parstoday.ir/sw/news/world-i61661-matumaini_baada_ya_watafiti_kugundua_dawa_ya_kutibu_corona
Matumaini yameenea kote duniani baada ya watafiti katika Chuo Kikuu cha Oxford cha Uingereza kutangaza kile walichokitaja kuwa ni ‘hatua kubwa' katika kuwatibu wagonjwa wa COVID-19 au corona.
(last modified 2023-11-27T12:14:11+00:00 )
Jun 17, 2020 11:14 UTC
  • Matumaini baada ya watafiti kugundua dawa ya kutibu corona

Matumaini yameenea kote duniani baada ya watafiti katika Chuo Kikuu cha Oxford cha Uingereza kutangaza kile walichokitaja kuwa ni ‘hatua kubwa' katika kuwatibu wagonjwa wa COVID-19 au corona.

Watafiti hao wamebaini kuwa dawa aina ya steroidi dexamethasone ina  uwezo wa kuepusha hatari ya kifo miongoni mwa wagonjwa mahututi.
Utafiti uliofanywa kwa zaidi ya wagonjwa 2,000, umeonyesha kuwa dawa hiyo ilipunguza hatari ya mgonjwa kufa kutoka asilimia 40 hadi asilimia 28, haswa wagonjwa ambao hawangeweza kupumua bila usaidizi wa mashine.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limetoa taarifa na kutangaza kufurahishwa na matokeo ya awali ya najaribio ya dawa hiyo  ya kutibu corona Uingereza 
Kwa wagonjwa wanaotumia mashine za kupumua, dawa hiyo ilionesha kwamba imepunguza idadi ya vifo kwa theluthi moja, na kwa wagonjwa wanaohitaji hewa ya oksijeni, idadi ya vifo ilipungua kwa humusi au moja ya tano kulingana na matokeo ya awali yaliyotolewa na WHO.
Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus amesema hii ndio dawa ya kwanza kupunguza idadi ya vifo kwa wagonjwa wa virusi vya corona wanaohitaji oksijeni au walio kwenye mashine za kupumua.
Dexamethasone ni dawa ambayo imekuwa ikitumiwa kwa muda kupunguza uvimbe katika hali tofauti kama vile ugonjwa wa saratani, yabisi kavu na kadhalika.
Hadi sasa hakuna chanjo ambayo imepatikana kukabili virusi vya corona.

Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus

Ugonjwa wa COVID-19 uliibuka kwa mara ya kwanza Disemba mwaka 2019 mjini Wuhan nchini China na sasa umeenea kote duniani.
Idadi jumla ya walioambukizwa COVID-19 duniani hadi kufikia Alhamisi hii ilikuwa ni takribani milioni 7.94 na waliopoteza maisha ni zaidi ya 535,000.
Marekani inaongoza duniani kwa maambukizi na vifo vya corona ambapo hadi kufikia leo watu  zaidi ya milioni 2. 8 walikuwa wameambukizwa COVID-19 na wengine wasiopungua 119,000 wamepoteza maisha.