Uungaji mkono wa nchi za Ulaya kwa utawala wa Kizayuni, wapungua
Jinai zilizofanywa na utawala wa Kizayuni katika mashambulizi ya hivi karibuni kwenye Ukanda wa Ghaza huko Palestina zimepelekea kupungua uungaji mkono wa nchi za Ulaya kwa dola katili la Israel.
Kwa mujibu wa televisheni ya al Jazeera ya Qatar, matokeo ya uchunguzi wa maoni uliofanywa na taasisi ya YouGov ya Uingereza yanaonesha kuwa, uungaji mkono wa nchi za Ulaya kwa utawala wa Kizayuni umeporomoka sana katika mwezi Februari mwaka huu.
Kwa mujibu wa uchunguzi huo, uungaji mkono wa nchi za Uingereza, Ufaransa na Denmark kwa utawala wa Kizayuni wa Israel uliporomoka kwa nukta 27, 23 na 22 kwa utaratibu ikilinganishwa na mwanzoni mwa mwaka huu.
Jinai za hivi karibuni za Israel dhidi ya Wapalestina hasa wa Ukanda wa Ghaza zimepokewa kwa hasira na watu wengi duniani na kumefanyika maandamano makubwa katika pembe mbalimbali za dunia kulaani jinai hizo.
Kuanzia tarehe 10 mwezi uliopita wa Mei, utawala wa Kizayuni wa Israel ulianzisha mashambulio makubwa ya kikatili dhidi ya Wapalestina wa Ukanda wa Ghaza kwa muda wa siku 12. Wapalestina 248 wakiwemo watoto wadogo 69, wanawake 39 na vizee 17 waliuliwa shahidi na Wazayuni kwenye jinai hizo. Wapalestina wengine 1,910 walijeruhiwa kwenye ukatili huo.
Baada ya kupita siku 12 za jinai hizo, baraza la mawaziri la Israel liliomba kusimamishwa mashambulio ya makombora na maroketi yaliyofanywa na wanamapambano wa Palestina kujihami na jinai hizo za Wazayuni. Kikao cha baraza hilo la mawaziri la utawala wa Kizayuni kilifanyika kwa masaa matatu na mwishowe mawaziri wote waliomba kwa kauli moja kusimamishwa vita hivyo.