Putin: Ushirikiano wetu na Pakistan utaimarisha usalama wa kikanda
(last modified Sun, 14 Aug 2022 11:24:59 GMT )
Aug 14, 2022 11:24 UTC
  • Putin: Ushirikiano wetu na Pakistan utaimarisha usalama wa kikanda

Rais Vladimir Putin wa Russia amewatumia ujumbe viongozi wa Pakistan na kuwahakikishia kuwa ushirikiano baina ya nchi zao utaimarisha usalama katika ukanda huu mzima.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Sputnik, Putin alituma ujumbe huo jana kwa viongozi wa ngazi za juu wa Pakistan akiwemo Rais Arif Alvi,  Waziri Mkuu Shehbaz Sharif pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani wa Pakistan, Rana Sanaullah Khan, akiwapa mkono wa pongezi kwa maadhimisho ya mwaka wa 50 wa kuundwa nchi ya Pakistan na kuelezea matumaini yake kwamba ushirikiano wa Moscow na Islam Abad utaongezeka na kuimarisha utulivu na amani katika eneo hili zima.

Katika ujumbe wake huo, Putin ametilia mkazo ushirikiano baina ya Russia na Pakistan katika masuala muhimu yanayozihusu moja kwa moja nchi hizo mbili kama kadhia ya Afghanistan na vita dhidi ya ugaidi.

Rais Arif Alvi wa Pakistan, 

 

Uhusiano wa Pakistan na Russia umeingia katika hali nyeti na muhimu sana baada ya waziri mkuu wa zamani wa Pakistan, Imran Khan kusema kuwa, vibaraka wa Marekani walikula njama za kumpindua huko Pakistan kutokana na misimamo yake kuhusu Russia ambayo inakinzana na manufaa ya Marekani katika eneo hili.

Mara zote Imran Khan anasema, sababu ya kung'olewa kwake madarakani ni njama za Marekani na vibaraka wake wa ndani ya Pakistan ambao ndio walioko madarakani hivi sasa na kwamba hajuti kwa msimamo wake huo wa kupinga ubeberu wa Marekani.