Ijumaa, Mei 11, 2018
Leo ni Ijumaa tarehe 24 Sha'ban 1439 Hijiria, inayosadifiana na tarehe 11 Mei 2018 Miladia.
Siku kama ya leo miaka 322 iliyopita, yaani tarehe 11 Mei mwaka 1696 Miladia, alifariki dunia mwandishi na mwanafikra wa Kifaransa, Jean de La Bruyère. De la Bruyère alizaliwa mwaka 1645 Miladia, na kuwa wakili baada ya kutabahari katika elimu ya sheria. Hata hivyo baadaye aliachana na kazi ya uwakili na akaanza kufanya kazi serikalini, huku akijifunza masuala ya maadili na tafakuri ya mwanadamu katika zama zake. Mwandishi huyo wa Kifaransa ameandika vitabu vingi vinavyohusu utamaduni, mila na mienendo ya mwanadamu. Kadhalika ametoa mchango mkubwa katika uga wa fasihi ya Kifaransa.
Siku kama ya leo miaka 154 iliyopita alizaliwa Ethel Lilian Voynich mwandishi wa Ki-Ireland. Akiwa na umri wa miaka 21, Bi Lilian alielekea Russia na kusoma fasihi ya lugha ya Kirusi. Ni katika kipindi hicho ndipo alipoanza taratibu kuwa na shauku na fani ya uandishi na fasihi ya lugha. Bi Ethel Lilian aliaga dunia mwaka 1960.
Siku kama ya leo, miaka 151 iliyopita, sawa na tarehe 11 mwezi Mei mwaka 1867 Miladia, iliundwa nchi ya magharibi mwa bara Ulaya ya Luxembourg. Awali Luxembourg ilifahamika kama Lutxenbourg katika karne ya 10 hadi 15, ikiwa sehemu ya Utawala wa Roma. Hadi katikati ya karne ya 19, nchi hiyo ilikuwa ikiendeshwa na serikali na watawala wa madola yaliyokuwa na nguvu na ushawishi wakati huo Ulaya. Luxembourg ambayo imezungukwa na Ubelgiji, Ufaransa na Ujerumani, ilitangazwa kuwa nchi huru katika Kongamano la London lililofanyika Mei 11 mwaka 1867 katika mji huo mkuu wa Uingereza na kuanza kutambulika kimataifa.
Siku kama ya leo miaka 127 iliyopita, alifariki dunia Ayatullah Mirza Mohammad Hassan Shirazi, mmoja wa mafaqihi na marjaa wakubwa wa ulimwengu wa Kiislamu. Alizaliwa mwaka 1230 Hijiria mjini Shirazi, moja ya miji ya kusini mwa Iran na baada ya kuhitimu masomo yake ya msingi alielekea mjini Najaf, lraq na kujiunga na hauza ya kielimu mjini hapo ambapo alichukua muda mrefu akisoma kwa maulama wakubwa akiwemo Sheikh Murtadha Answari, mmoja wa maulama watajika wa Kiislamu zama hizo. Ni baada ya hapo ndipo Ayatullah Mirza Mohammad Hassan Shirazi alitokea kuwa mmoja wa walimu wakubwa katika uga huo. Ayatullah Mirza Mohammad Hassan Shirazi alipata umashuhuri nchini Iran baada ya kutoa fatwa ya kupiga marufuku uvutaji sigara, katika hatua za kukabiliana na mkoloni Mwingereza suala ambalo lilitoa pigo kubwa kwa mkoloni huyo.
Siku kama ya leo miaka 113 iliyopita, Salvador Felipe Dali, mchoraji na mchongaji wa sanamu za mawe na mtaalamu wa sanaa ya maandishi au Graphic Arts wa Kihispania alizaliwa. Alianza kuonyesha kipaji chake katika sanaa ya uchoraji akiwa kijana mdogo na kwa muda mfupi tu akawa mashuhuri kimataifa. Salvador Felipe Dali alikuwa na kipaji cha aina yake na ubunifu katika taaluma hizo na ndiye anayehesabiwa nchini Uhispania kuwa mwasisi wa uchoraji wa kisasa. Mwanasanaa huyo stadi aliaga dunia mwaka 1989.
Siku kama ya leo miaka 83 iliyopita kituo cha kwanza cha kurushia matangazo ya televisheni kwa jina la Nipkow kilianza kazi rasmi katika mji wa Berlin huko Ujerumani, hatua ambayo iliwawezesha watu kuanza kutumia runinga au televisheni. Kituo hicho cha kwanza cha matangazo ya televisheni kilipewa jina la Nipkow kwa shabaha ya kumuenzi Paul Gottlieb Nipkow ambaye alikuwa miongoni mwa wavumbuzi asili wa televisheni. Nipkow alivumbua njia ya kubadili picha na kuwa mawimbi na kisha kuyarejesha mawimbi hayo katika sura ya picha.
Na siku kama ya leo miaka 78 iliyopita, majeshi ya pamoja ya Ufaransa na Uingereza yaliwasili nchini Ubelgiji kwa ajili ya kuisaidia nchi hiyo iliyokuwa ikikabiliwa na uvamizi wa vikosi vya Ujerumani ya Kinazi. Hatua hiyo ya Ufaransa na Uingereza ya kuiunga mkono Ubelgiji ilikuwa ni kwa mujibu wa makubaliano yaliyokuwako baina yao. Licha ya kuweko muungano huo wa kijeshi, vikosi vya Ujerumani ya Kinazi mbali na kuyashinda majeshi ya Ubelgiji yalivishinda pia vikosi vya pamoja vya Uingereza na Ufaransa na kuikalia kwa mabavu ardhi yote ya nchi hiyo.