Oct 29, 2019 02:51 UTC
  • Jumanne, tarehe 29 Oktoba, 2019

Leo ni tarehe 30 Safar 1441 Hijria inayosadifiana na tarehe 29 Oktoba mwaka 2019.

Katika siku ya mwisho ya mwezi wa Safar miaka 1237 iliyopita, aliuawa shahidi Imam Ali bin Mussa ar Ridha AS, mmoja kati ya wajukuu wa Mtume Mtukufu SAW. Mtukufu huyo alizaliwa mwaka 148 Hijria katika mji wa Madina na alichukua jukumu la kuongoza Umma wa Kiislamu baada ya kuuawa shahidi baba yake, yaani Imam Mussa al Kadhim AS. Mnamo mwaka 200 Hijria, Maamun, Khalifa wa Bani Abbasi, alimtaka Imam Ridha AS aelekee kwenye makao ya Khalifa huyo yaliyokuwa katika mji wa Marwi, kusini mashariki mwa Turkemenistan ambayo ilikuwa sehemu ya Khorasan Kuu. Ijapokuwa kidhahiri Maamun alimfanya Imam Ridha kuwa mrithi wake, lakini kwa njia hiyo alikusudia kuimarisha zaidi nguvu za utawala wake. Utukufu na daraja ya juu ya kielimu na kimaanawi aliyokuwa nayo Imam Ridha na ushawishi wake uliokuwa ukiongezeka siku hadi siku ndani ya fikra na nyoyo za watu, vilimtia woga na hofu Maamun, na hivyo akaamua kufanya njama za kumpa sumu na kumuua shahidi Imam Ridha katika siku kama leo. Imam AS amesema:"Mja bora zaidi ni yule ambaye kila anapofanya jema hufurahia, na kila anapokosea huomba msamaha, inapomfikia neema hushukuru, anapokumbana na masaibu husubiri na wakati anapoghadhibika husamehe".

Haram ya Imam  Ridhaa (as), Mash'had Iran

Siku ya mwisho ya mwezi Safar miaka 1440 iliyopita kulitokea tukio la Lailatul Mabiit na kuanza kwa hijra ya Mtume kutoka Makka kwenda Madina. Suala la hijra na kutoka Makka kuhamia Madina liliainishwa katika Baia ya Pili ya Aqaba. Makafiri wa Kikuraishi wa Makka walipopata habari hiyo walichukua uamuzi wa kumuua Mtume Muhammad (saw) na kwa sababu hiyo waliafiki pendekezo lililotolewa na Abu Jahl juu ya namna ya kutekeleza njama hiyo chafu. Kwa mujibu wa pendekezo hilo, kila ukoo kati ya koo zote za kabila la Kuraish lilitakiwa kumchagua kijana mmoja na wote kwa pamoja wavamie nyumba ya Mtume (saw) wakati wa usiku na kumuua akiwa amelala kitandani. Hata hivyo Mwenyezi Mungu SW alimjulisha Mtume wake kuhusu njama hiyo ya Makuraish na kumuamuru ahamie Madina usiku huo. Ili kuwapotosha makafiri wa Makka, Mtume (saw) alimtaka Imam Ali bin Abi Twalib (as) alale kitandani kwake. Usiku huo unajulikana katika historia kwa jina la Lailatul Mabiit kwa maana ya usiku ambao Ali bin Abi Twalib alikubali kuhatarisha maisha yake na kulala kwenye kitanda cha Mtume Muhammad (saw) huku akijua kwamba Makuraishi watavamia nyumba hiyo na kumkata kwa mapanga mtukufu huyo.

Katika siku kama ya leo miaka 96 iliyopita, mfumo wa utawala wa serikali ya jamhuri uliasisiwa nchini Uturuki kwa uongozi wa Rais Mustafa Kemal mashuhuri kwa jina la Ataturk. Kemal Ataturk aliiongoza kidikteta nchi hiyo kwa muda wa miaka 15 na kufanya hujuma za kufuta sheria, nembo pamoja na matukufu ya Kiislamu na wakati huo huo, kueneza utamaduni na nembo za Kimagharibi nchini humo. Hata baada ya kufariki dunia kiongozi huyo aliyekuwa na uadui na Uislamu mnamo mwaka 1938, njama hizo dhidi ya Uislamu nchini Uturuki ziliendelezwa na wafuasi wake.

Mustafa Kemal Ataturk

Siku kama ya leo miaka 93 iliyopita yaani tarehe 7 Aban mwaka 1305 Hijria Shamsia Ayatullah Sayyid Hassan Modarres aliyekuwa miongoni mwa wanazuoni na wanamapambano maarufu nchini Iran alinusurika jaribio la kuuawa. Jaribio hilo lilifanywa na vibaraka wa Shah Reza Pahlavi aliyekuwa maarufu kwa udikteta, ukatili na upinzani mkubwa dhidi ya maulama wa Kiislamu. Uhasama wa utawala wa kifalme wa Pahlavi dhidi ya Ayatullah Modarres ulitokana na mchango mkubwa wa mwanazuoni huyo wa Kiislamu katika kuwaamsha wananchi na kufichua njama za utawala wa Kipahlavi na muungaji mkono wake yaani serikali ya Uingereza. Kwa kipindi fulani Ayatullah Modarres alikuwa mwakilishi wa wananchi wa Tehran katika Bunge. Baada ya kunusurika kifo katika jaribio hilo Ayatullah Modarres alipelekwa uhamishoni kwa amri ya mfalme dikteta Reza Khan na muda mfupi baadaye aliuawa shahidi na vibaraka wa Shah.

Ayatullah Sayyid Hassan Modarres

Siku kama ya leo miaka 63 iliyopita, askari jeshi wa utawala wa Kizayuni wa Israel walishambulia Peninsula ya Sinai iliyoko Misri. Mashambulio hayo yalianza baada ya Rais wa wakati huo wa Misri, Gamal Abdul Nassir kutaifisha mfereji wa Suez. Siku mbili baada ya mashambulio hayo, Uingereza na Ufaransa zilipeleka majeshi yao pembezoni mwa mfereji huo kwa lengo la kuusaidia utawala ghasibu wa Israel. Mnamo mwaka 1957 majeshi vamizi ya Ufaransa, Uingereza na utawala haramu wa Israel yaliondoka katika ardhi ya Misri kufuatia mashinikizo ya fikra za waliowengi, madola mengi ya Magharibi na upatanishi wa Umoja wa Mataifa.

Na siku kama ya leo miaka 63 iliyopita, katika jinai yao nyingine, Wazayuni waliwauwa kwa umati wakazi wa kijiji cha Kafr Qasim huko Palestina. Wanajeshi wa utawala wa Kizayuni walitangaza utawala wa kijeshi katika kijiji hicho. Wanajeshi wa utawala wa Kizayuni waliwauwa kwa umati wanawaume, wanawake na watoto madhlumu wa Palestina wasiopungua 49 na kujeruhi makumi ya wengine huko Kafr Qasim. 

Msikiti wa Mashahidi, Kafr Qasim

 

Tags