Jumatano, Juni 1, 2016
Leo ni Jumatano tarehe 25 Shaaban mwaka 1437 Hijiria, inayosadifiana na Juni 1 2016 Miladia
Miaka 1300 iliyopita katika siku kama ya leo, yaani tarehe
25 Shaaban mwaka 137 Hijria Qamaria, Abu Muslim Khorassani, kamanda Muirani,
aliuawa kwa amri ya Mansour, mtawala wa wakati huo wa Ukhalifa wa Bani Abbas.
Abul Muslim Khorassani alikuwa kiongozi wa mwamko uliojulikana kama "Siyah
Jamegan" katika eneo la Khorassan. Mwamko huo ulikuwa dhidi ya watawala wa
kiimla. Katika kipindi kifupi, aliweza kupata wafuasi katika aghalabu ya miji
na vijiji. Abu Muslim na wafuasi wake walifanikiwa kuwashinda watawala wa Bani
Umayya. Kwa msingi huo, baada ya kuanguka utawala wa Bani Umaiyya ulikuja
madarakani utawala wa Bani Abbas. Hapo Abu Muslim alikuwa na nguvu na ushawishi
mkubwa kiasi cha Mansour, mtawala wa Bani Abbas kuingiwa na kiwewe na hivyo
akapanga njama ya kumuua. Baada ya kuuawa Abu Muslim, baadhi ya wafuasi wake
walianzisha mapigano ambayo yaliendelea kwa muda mrefu.
Siku kama ya leo miaka 30 iliyopita, wanafunzi kadhaa wa shule za msingi
waliwaandikia barua wenzao duniani kote na kuwataka kupitisha muda wao wa siku
nzima kwa ajili ya amani. Sehemu moja ya barua ya wanafunzi hao ilisomeka kama
ifuatavyo: "Wazazi wanatupenda, kwa kuwa sisi ni watoto wao. Hata hivyo
je, mnafahamu ni dunia ya aina ngani waliyotuandalia? Sisi kamwe tusingekuwa na
fursa ya kukua, iwapo wazazi wetu wangefanya kosa japo dogo tu. Tunahitaji
suhula kwa ajili ya kukua na malezi." Kwa ajili hiyo, siku ya kwanza ya mwezi
Juni kila mwaka, ikapewa jina la "Siku ya Watoto Duniani". Kwa ajili
hiyo marasimu maalumu hufanyika katika pembe mbalimbali duniani katika
kuadhimisha siku hiyo.
Miaka 46 iliyopita, siku kama ya leo, alifariki dunia nchini
Iraq Ayatullahi Sayyid Muhsin Hakim mtaalamu wa fiq'hi, msomi mkubwa na mmoja
wa maraajii wakubwa wa Kiislamu. Alizaliwa mwaka 1264 Hijiria Shamsia.
Ayatullah Hakim alipata kuhifadhi Qur'ani Tukufu akiwa na umri mdogo na baadaye
alisoma elimu ya dini kwa walimu wakubwa wa zama zake. Ayatullah Hakim
aliongoza mapambanao dhidi ya waliokuwa wakiupinga Uislamu na alitoa fatwa
kupinga Ukomunisti. Aidha alitoa fatwa kuhusu Jihadi dhidi ya utawa wa
Kizayuyni wa Israel. Kuna athari nyingi kutoka kwa Sayyid Hakim, miongoni mwazo
ni pamoja na kitabu kiitwacho "Mustamsikul Urwatul Wuthqaa" kilicho
katika juzuu 14, "Haqaiqul Usul" na " Nahjul Fuqaha."
Na siku kama ya leo miaka 64 iliyopita, aliaga dunia John Dewey, msomi na
mwandishi mashuhuri wa Marekani. Dewey alizaliwa 20 Oktoba mwaka 1859 na
alikuwa amebobea mno katika elimu ya malezi na aliweza kujifunza mengi
alipokuwa katika chuo kikuu cha Colombia. John Dewey alifanikiwa kuandika
vitabu vingi kuhusiana na malezi na makuzi ya mtoto. Miongoni mwa vitabu
mashuhuri alivyoviandika katika kipindi cha uhai wake ni pamoja na "How we
think", "The Public and its Problems" na "Freedom and
Culture." John Dewey alifariki dunia mwaka 1952 akiwa na umri wa miaka 93.