Serikali ya Tanzania yatakiwa kubuni sheria maalumu ya ukatili dhidi ya wanawake
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i111830-serikali_ya_tanzania_yatakiwa_kubuni_sheria_maalumu_ya_ukatili_dhidi_ya_wanawake
Serikali ya Tanzania imetakiwa kubuni sheria maalumu ya kukabiliana na ukatili dhidi ya wanawake.
(last modified 2026-01-14T08:12:18+00:00 )
May 16, 2024 08:50 UTC
  • Serikali ya Tanzania yatakiwa kubuni sheria maalumu ya ukatili dhidi ya wanawake

Serikali ya Tanzania imetakiwa kubuni sheria maalumu ya kukabiliana na ukatili dhidi ya wanawake.

Watetezi wa haki za binadamu nchini Tanzania wameitaka serikali ya nchi hiyo kubuni sheria maalumu kwa ajili ya kupambana na ukatili dhidi ya wanawake na wasichana kutokana na kuwepo kwa ongezeko la kubwa la ukatili katika kipindi cha hivi karibuni hali inayoendelea kutia wasiwasi.

Watetezi wa haki za binadamu nchini Tanzania wanasema kuwa,  sheria iliyopo bado ina mapungufu yanayoendelea kutoa nafasi ya wanawake kuendelea kufanyiwa ukatili.

Ukatili dhidi ya wanawake na wasichana ni miongoni mwa changamoto ambayo inaendelea kushuhudiwa sehemu mbali mbali nchini Tanzania, ukatili huo ukihusisha wa kimwili, kijinsia, kisaikolojia, na hata unyanyasaji wa wanandoa ambapo unaonekana kuongezeka.

 

Kwa mujibu wa ripoti ya Mkurugenzi wa Uchunguzi wa Jinai (DCI) ni kuwa, katika kipindi cha miaka mitano (2018-2022) nchini Tanzania wanawake 2,438 walipoteza maisha yao kutokana na ukatili ikiwa ni sawa na wanawake 492 kwa mwaka na wanawake 43 kwa mwezi huku kwa mwaka 2023 ukionyesha ongezeko la wanawake 53 wanaofariki kila mwezi hali inayoleta wasiwasi.

Getrude Biabene ni Afisa mwandamizi wa masuala ya jinsia, wanawake, na watoto katika Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) anaeleza sababu ambayo imepelekea kuwepo kwa ongezeko la vitendo vya mauaji kwamba, ni kutokana na watu kupitia vitendo vya ukatili na kutotoa taarifa mapema pamoja na mifumo ya haki anmbayo haitoi msaada wa haraka kwa wanaopitia vitendo vya ukatili.