Wananchi wa Burundi waendelea kufanya maandamano dhidi ya Ufaransa
Wananchi wa Burundi wameendelea kufanya maandamano dhidi ya Ufaransa ambapo leo walikusanyika mbele ya ubalozi wa Ufaransa mjini Bujumbura.
Maandamano hayo yaliyojumuisha maelfu ya raia katika mji wa Burundi yanapinga azimio la hivi karibuni la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa la kutumwa askari polisi waangalizi katika nchi hiyo ambayo kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa inashuhudia mvutano wa kisiasa.
Maandamano hayo yaliyoanza tangu siku ya Jumamosi yanalalamikia pendekezo la mwakilishi wa Ufaransa katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa la kutumwa nchini Burundi ambalo hatimaye lilipasishwa na nchi wanachama.
Katika kikao cha Ijumaa iliyopita baraza hilo liliafiki kutumwa maafisa wa polisi 228 katika mji wa Bujumbura na miji mingine nchini Burundi kwa muda wa mwaka mmoja. Nchi 11 wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa zilipiga kura ya kuunga mkono azimio hilo lililoandaliwa na Ufaransa, huku nchi nne za China, Misri, Angola na Venezuela zikijizuia kupigia kura.
Polisi hao wa Umoja wa Mataifa watakuwa na jukumu la kulinda usalama sambamba na kusimamia haki za binaadamu kwa ushirikiano na waangalizi wa kimataifa na wataalamu wa masuala ya kijeshi wa Umoja wa Afrika nchini humo.
Awali serikali ya Bujumbura ilikubali pendekezo la Umoja wa Afrika la kutumwa askari 50 tu wa UN pamoja na waangalizi 100 wa umoja huo
Itakumbwa kuwa, Burundi ilitumbukia kwenye mgogoro wa kisiasa kufuatia hatua ya chama tawala CNDD-FDD kumuidhinisha Rais Pierre Nkurunziza wa nchi hiyo kugombea muhula wa tatu katika uchaguzi uliopita, machafuko ambayo hadi sasa yamesababisha mauaji ya watu zaidi ya 500 huku wengine zaidi ya laki 2 na 70 elfu wakilazimika kuitoroka nchi na kuwa wakimbizi.